Serikali kufanya mazungumzo na wafadhili

By Grace Mwakalinga , Nipashe Jumapili
Published at 05:30 PM Nov 23 2025
Msemaji Mkuu wa Serikali ambaye pia ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Gerson Msigwa
PICHA: MTANDAO
Msemaji Mkuu wa Serikali ambaye pia ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Gerson Msigwa

Serikali imesema itafanya mazungumzo na wafadhili ambao wameonyesha nia ya kujitoa kufadhili miradi mbalimbali nchini kufuatia matukio yaliyotokea Oktoba 29,2025 wakati wa uchaguzi mkuu.

Kauli hiyo imetolewa na Msemaji Mkuu wa Serikali ambaye pia ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Gerson Msigwa wakati wa Mkutano na Waandishi wa Habari jijini Dar es Salaam.

Amesema  baadhi ya wafadhili  wameonyesha wasiwasi  kutokana na yaliyotokea wakati wa uchaguzi , lakini akasisitiza kuwa mazungumzo yanaendelea  wanatumaini watafikia  makubaliano. “Ni kweli kutakuwa na mtikisiko katika maeneo fulani kiuchumi, Serikali inatambua hali hiyo na tupo tayari kuhakikisha mambo hayakwami,” amesema.

Ameeleza kuwa licha ya baadhi ya wadau kutangaza kusitisha ufadhili, miradi mingi ya maendeleo nchini inaendelea kutekelezwa kwa fedha za ndani. Hivyo, juhudi za Serikali katika kuwaletea wananchi maendeleo hazitasimama.

Ameongeza kuwa Serikali imejiandaa kukabiliana na athari zozote zitakazojitokeza ili kuhakikisha wananchi wanaendelea kupata huduma muhimu bila usumbufu. “Serikali inawajali wananchi  wake ipo makini na itahakikisha inasimamia  maslahi ya Taifa na kuendeleza miradi yote muhimu,” amesema