CATC inatarajia kutumia 78 bn/- kwa ajili ya ujenzi wa chuo chake jijini Dar

By Mwandishi Wetu , Nipashe
Published at 02:23 PM Jul 09 2024
Ramani ya ujenzi wa Chuo cha Usafiri wa Anga nchini (CATC).
Picha: Mpigapicha Wetu
Ramani ya ujenzi wa Chuo cha Usafiri wa Anga nchini (CATC).

Chuo cha Usafiri wa Anga nchini (CATC) ambacho ni Chuo cha Mafunzo cha Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) kimesema kuwa wamepanga kutumia zaidi ya bilioni 78 kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya chuo chake kitakachojengwa jijini Dar es Salaam.

Akizungumza jijini Dar es Salaam wakati wa Maonyesho ya 48 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (DITF) yanayoendelea, Afisa Uhusiano na Masoko wa CATC, Ally Changwila amesema kuwa mradi wa ujenzi huo unagharamiwa na serikali kwa asilimia 100 kwa gharama ya zaidi ya bilioni 78 za Kitanzania na tayari serikali imeshatoa 5bn/- katika mwaka wa fedha uliopita ambazo zilitumika kwenye upembuzi yakinifu.

“Katika mwaka huu wa fedha, Serikali imetenga Shilingi bilioni 23 kwa ajili ya mradi huu utakaogharimu zaidi ya Shilingi bilioni 78 hadi kukamilika kwake katika eneo la hekta 18 lililopo Banana Dar es Salaam jirani na Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA). " alisema.

Changwila ambaye pia ni Ofisa Uhusiano Mkuu wa TCAA alisema kuwa mradi huo wa ujenzi utachukua miaka mitatu hadi kukamilika.

"Kutokana na mahitaji makubwa ya wataalamu wa usafiri wa anga, sisi kama CATC, tunazalisha rasilimali watu wenye ubora wa kimataifa ili kukuza maendeleo ya sekta hii ya usafiri wa anga. Tunawakaribisha wanafunzi kujiunga na Chuo chetu ili waweze kufikia ndoto zao za kufanya kazi kwa sekta hii,” alisema.

Ramani ya ujenzi wa Chuo cha Usafiri wa Anga nchini (CATC).

Aliongeza: “Kozi zetu zinatambulika kitaifa na kimataifa na wanafunzi wanaosoma hapa na kufaulu wanao uwezo wa kufanya kazi nchi yeyote duniani.”

Kwa upande wake Mkufunzi Mkuu wa CATC Thamarat Abeid alisema kuwa Chuo hicho cha Mafunzo ya Usafiri wa Anga kutokana na kutoa mafunzo yenye ubora wa hali ya juu kimeweza kupatiwa ithibati kutoka mamlaka mbalimbali za ndani na nje ya nchi ili kuweza kutoa kozi za usafiri wa anga,
“Tuna kibali cha kutoa mafunzo kutoka ISO 9001:, na vile vile ni wanachama kamili wa ICAO, TRAINAIR PLUS Gold.

Pamoja na hayo, tumesajiliwa na Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi (NACTVET ), Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania, Shirika la Mafunzo la Afrika (ATO) na sisi pia ni Mwanachama wa Shirika la Chartered Institute of Logistics and Transport (CILT), London, Kituo cha Mafunzo ya Usalama wa Anga (ASTC)," alisema. 

Abeid aliongeza: “Kutokana na programu zetu za mafunzo kuwa bora na zenye kukidhi mahitaji ya sekta ya anga, hivi karibuni tumepokea wanafunzi kutoka Botswana waliokuwa hapa kupata mafunzo na pia tumesaini Mkataba wa Makubaliano na Mamlaka ya Usafiri wa Anga ya Guinean Conakry ili kuwaleta wanafunzi wao ili waweze kupata mafunzo ya usafiri wa anga.”

Aliendelea zaidi kusema kwamba Chuo cha CATC ambacho kilianzishwa kama tawi la mafunzo la TCAA tarehe 10 Juni 1985 sasa ni mojawapo ya Taasisi bora zaidi za Mafunzo ya Usafiri wa Anga Duncan.

"Kutokana na ubora wa mafunzo tunayotoa, sasa ni miongoni mwa nchi 9 barani Afrika na 35 duniani kama Taasisi kutoa  Mafunzo ya Usalama wa Usafiri wa Anga," alisema.