Masauni ahimiza mbinu dhidi ya mabadiliko tabianchi

By Mwandishi Wetu , Nipashe Jumapili
Published at 03:10 PM Mar 23 2025
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira, Hamad Masauni
Picha: Mpichapicha Wetu
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira, Hamad Masauni

WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Hamad Masauni amewahimiza Watanzania kutumia nishati safi kupikia, ikiwa ni mkakati wa kupambana na mabadiliko ya tabianchi, uharibifu wa mazingira na kuhifadhi viumbe hai.

Aliyasema hayo mwishoni mwa wiki, jijini Dar es Salaam, wakati wa futari aliyoiandaa pamoja na Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), kwa wadau mbalimbali.

“Tunapohimiza kuhusu mazingira hatufanyi haya yote kwa ajili yetu wenyewe, bali kwa vizazi vitakavyokuja baada yetu kwa maana ya watoto na wajukuu zetu. 

Picha mbalimbali ya futari iliyoandaliwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira, Hamad Masauni kwa kushirikiana na Baraza la Taifa la Hufadhi na Usimamizi wa Mazingira NEMC Jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki
"Ni muhimu tuendelee kushirikiana, kufanya kazi pamoja na kufanya maamuzi ya pamoja ambayo yananufaisha mazingira na watu wanaoyategemea mazingira ambao kwa ujumla ni sisi wenyewe,” alisema.

Alisema wadau mbalimbali wana wajibu wa kutengeneza dunia endelevu na yenye maelewano kwa wote, huku akisisitiza umuhimu wa kulinda rasilimali zilizopo kwa kuhakikisha zinaendelea kuwapo, kwa ajili ya watoto  na vizazi vijavyo.

Pia, alisema kila mtu anatakiwa kuzingatia jinsi matendo yake, hata yawe madogo kiasi gani katika uhifadhi wa mazingira, kwa kuwa yanaweza kuwa na athari kubwa sana kwa mazingira.

Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Dk. Immaculate Semesi alisema kazi inayofanywa na wadau mbalimbali katika kuhifadhi, kulinda na kusimamia mazingira, ni faida kubwa kwa mazingira katika kutimiza maandiko ya vitabu vitakatifu.

“Sote tunajua Tanzania imebarikiwa kuwa na maliasili na mifumo ikolojia ya kipekee ambayo ni pamoja na aina nyingi za mimea, wanyama, wadudu, ndege tunatakiwa kuhakikisha tunapunguza athari za mabadiliko ya tabianchi.

“Kudhibiti shughuli za kibinadamu zinazoharibu mazingira kama uchimbaji madini, ufugaji na kilimo visivyo endelevu na ukataji mkubwa wa misitu,” alisema.

Alisema juhudi za pamoja ni kuhakikisha kwamba, aina hizo tofauti za uharibifu zinapunguzwa ama kumalizwa kabisa na kwamba hilo ndilo lengo ambalo serikali kupitia NEMC inajitahidi kufikia.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira, Hamad Masauni kwa kushirikiana na Baraza la Taifa la Hufadhi na Usimamizi wa Mazingira NEMC Jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki
Dk, Semesi pia alizungumzia Siku ya Kimataifa ya Kuondoa Taka, huku NEMC ikiandaa kuiadhimisha kuanzia Machi 28 hadi 30, 2025.

Alisema tukio hilo lililopangwa kufanyika katika Viwanja vya Mnazi Mmoja, jijini Dar es Salaam ni mahususi kwa kuyaleta pamoja makundi mbalimbali ya wadau wa mazingira, kwa lengo la kuangazia umuhimu wa usimamizi endelevu wa taka na kukuza uchumi mzunguko (promote a circular economy).

Alisema kauli mbiu ya mwaka huu ni "Kufikia lengo la taka sifuri katika masuala ya mitindo na nguo" na kauli mbiu ya Kitaifa ni "TAKA NI FURSA".

Washiriki wa futari hiyo
“Hii itakuwa ni fursa nyingine nzuri kwetu sote kukutana tena na kuendelea kuimarisha ushirikiano wetu katika kutafuta suluhisho la pamoja la changamoto za kimazingira zinazotukabili,” alisema.

Aliongeza kwamba mbali na jitihada zinazofanywa, serikali imepiga hatua katika kuhakikisha mazingira yanalindwa na yanahifadhiwa vizuri, ili kuendelea kutoa huduma na bidhaa zinazohitajika kwa kufanya tathmini ya athari za kimazingira na kijamii.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira, Hamad Masauni (katikati), kwa kushirikiana na Baraza la Taifa la Hufadhi na Usimamizi wa Mazingira NEMC Jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki
Alisema serikali imeweka mikakati mbalimbali   kuhakikisha sheria za mazingira na kanuni zake zinazingatiwa na wale wanaokiuka wanaadhibiwa kwa mujibu wa sharia zilizopo.

Pia, alisema wanafanya  tafiti za mazingira na usimamizi wa maeneo maalum, kusaidia uhamasishaji na programu za kuelimisha umma na kutambua kuwa mazingira ni suala mtambuka, majukumu ya usimamizi wa mazingira yanatakiwa kutekelezwa na takriban kila sekta kupitia sheria, kanuni, mikakati na mipango ya kisekta.