Mbunge Vita Kawawa akabidhi vifaatiba vyenye thamani ya Sh milioni 14.9

By Gideon Mwakanosya , Nipashe Jumapili
Published at 09:58 AM May 11 2025
Mbunge Vita Kawawa akifungua Zahanati ya kijiji cha Luhangano Namtumbo
PICHA: MTANDAO
Mbunge Vita Kawawa akifungua Zahanati ya kijiji cha Luhangano Namtumbo

Wananchi wa kijiji Luhangano kata ya Mputa wilaya ya Namtumbo wameiomba serikali kuona umuhimu wa kuwasaidia kuwapelekea huduma ya nishati ya umeme katika zahanati ya kijiji hicho iliyozinduliwa na mbunge wa jimbo la Namtumbo, Vita Kawawa mwishoni mwa wiki.

Ombi hilo lilitolewa mwishoni mwa wiki na diwani ya kata ya Mputa, Swalehe Moto kwenye hafla fupi ya uzinduzi wa zahanati hiyo na kuwakabidhi vifaa tiba vyenye thamani ya shilingi milioni 14.9 ambavyo vitasaidia kutoa huduma kwa wananchi wa kijiji hicho ambao awali walikuwa na tatizo kubwa la kutembea umbali mrefu kufuata huduma za afya katika vijiji vingine  vinavyotoa huduma ya afya.

Wananchi wakimsikiliza mbunge, Vita Kawawa

Moto ambaye ni mwenyekiti  wa kamati ya maendeleo  kata ya  Mputa alisema kuwa pamoja na kwamba serikali imesaidia  upatikanaji wa huduma mbalimbali za maendeleo bado kuna tatizo la  nishati ya umeme katika zahanati ya kijiji hicho hivyo aliiomba serikali kupitia Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kuona namna ya kuwasogezea huduma hiyo kwenye zanahati ili waganga pamoja na wahudumu wa afya waweze kuwahudumia wagonjwa kwa weledi zaidi.

Alisema kuwa mbunge wa jimbo la Namtumbo, Vita Kawawa amekuwa ni mwakilishi mzuri kwenye  bunge la jamhuri ya muungano wa tanzania  kwa kupigania maendeleo ya jimbo hilo kwani kwa upande wa kata ya mputa ina shule za msingi tano na sekondari moja ambayo inawafunzi wa kidato cha kwanza hadi kidato cha sita ambazo kwa juhudi za mbunge wao pamoja na serikali zimefanyiwa ukarabati mkubwa wa miundo mbinu ya madarasa pamoja na matundu ya vyoo.

Ofisa mtendaji wa kijiji cha Luhangano, Veronia Tembo alisema kuwa zahanati ya kijiji chao bado inahitaji kupatiwa vifaa tiba zaidi kwani eneo hilo lipo mbali na makao makuu ya kata na alimweleza mbunge kuwa iko haja ya kuona umuhimu wa kuwa karibu zaidi  na kijiji hicho ambacho kinahitaji zaidi  kutatuliwa changamoto zinazowakabili licha ya kuwa kijiji hicho kina maji ya mtiririko ambayo yanatosheleza baada ya mbunge  kusaidia kutatua tatizo la maji ambalo lilikuwa linawakabili wananchi kwa muda mrefu.