RCC yaridhia Jimbo la Solwa kugawanywa

By Marco Maduhu , Nipashe Jumapili
Published at 03:04 PM Mar 16 2025
Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Anamringi Macha, akizungumza kwenye kikao cha RCC, kupitisha na kuridhia mapendekezo ya kuligawa Jimbo la Solwa.
Picha: Marcdo Maduhu
Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Anamringi Macha, akizungumza kwenye kikao cha RCC, kupitisha na kuridhia mapendekezo ya kuligawa Jimbo la Solwa.

KIKAO cha Kamati cha Ushauri Mkoa wa Shinyanga (RCC), kimeridhia mapendekezo ya Tume huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), kuligawa Jimbo la Solwa, kuwa na majimbo mawili ya uchaguzi ambayo ni Solwa na Itwangi.

Kikao hicho kimefanyika, Machi 15, 2025, kikiongozwa na Mwenyekiti wake Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Anamringi Macha.

Macha, amesema baada ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), kutoa vigezo na mapendekezo kwa ajili ya kuligawa Jimbo la Solwa, kwamba kunapaswa kufuatwa taratibu zingine za vikao, kikiwamo Kikao cha Baraza cha Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga, kikao cha Kamati cha Ushauri Wilaya ya Shinyanga DCC na kikao cha Mkoa RCC, kupitisha mapendezo ya kuligawa jimbo hilo.

RCC yaridhia Jimbo la Solwa kugawanywa
Amesema vikao viwili tayari vilishafanyika, ambavyo ni Baraza la Madiwani na Kikao cha Kamati ya Ushauri wilaya ya Shinyanga (DCC) na sasa wamekaa Kikao cha Kamati ya Ushuari Mkoa (RCC) na wamepitia vigezo vyote vilivyotolewa na INEC, kwa ajili ya kuligawa jimbo la Solwa, kwamba vigezo vyote wamekidhi na wameridhia jimbo hilo ligawanywe.

“Kigezo cha kwamba kilichotolewa na Tume huru ya Taifa ya Uchaguzi ni Idadi ya watu, kwa mujibu wa sense ya watu na makazi mwaka 2022, jimbo hilo la Solwa lina watu 468,611, lakini takwimu za mwaka huu 2025, kuna ongezeko la watu 503,167, na ukigawanya jimbo la Solwa litakuwa na watu 309,821, na Itwangi 193,346, hivyo tumekidhi vigezo,” amesema Macha.“Kigezo kingine ni ukubwa wa eneo, Jimbo la Solwa lina ukubwa Kilomita za Mraba 4,212, eneo ambalo ni kubwa na lina kigezo jimbo hili kugawanywa,” ameongeza Macha.

RCC yaridhia Jimbo la Solwa kugawanywa
Aidha, amesema jimbo hilo litakapogawanywa, Jimbo la Solwa litakuwa na Kata 12 na Itwangi Kata 14, na kwamba kukiwa na Wabunge wawili kutasaidia wananchi kuwa karibu na Wabunge wao, huku akimpongeza Mbuge wa Solwa Ahmed Salum, kwa kuchapa kazi ya kuwahudumia wananchi wote wa jimbo hilo licha ya ukubwa wake.
RCC yaridhia Jimbo la Solwa kugawanywa
“Jimbo hilo la Solwa limekidhi vigezo vyote vya Tume huru ya Taifa ya Uchaguzi kuligawa, kuwe na majimbo mawili ya uchaguzi, Solwa yenyewe na Itwangi,kikao cha RCC kimeridhia Jimbo hili ligawanywe,” amesema Macha.

Amesema baada ya kikao hicho cha RCC kupitisha na kuridhia mapendekezo ya kuligawa Jimbo hilo la Solwa, taarifa zake zitapelekwa Tume huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) kabla ya tarehe Machi 26, mwaka huu.

Aidha, INEC, ilitangaza baadhi ya majimbo kugawanywa, na kuwa na majimbo mawili ya uchaguzi, likiwamo Jimbo la Solwa wilayani Shinyanga.