Wanaharakati: Juhudi kumkomboa mwanamke, ukatili kikwazo

By Grace Mwakalinga , Nipashe Jumapili
Published at 05:06 PM Mar 23 2025
Mkurugenzi Mtendaji wa TGNP, Lilian Liundi
Picha: MGrace Mwakalinga
Mkurugenzi Mtendaji wa TGNP, Lilian Liundi

LICHA ya Juhudi za serikali kuhusu haki za wanawake, suala la ukatili dhidi ya wanawake limeongezeka na kuchukuliwa kama janga.

Akizungumza Machi 21, 2025, kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani, wakati wa washilisho la Uchambuzi wa Mwelekeo wa Takwimu kwa maeneo matatu muhimu kutoka kwa Mpango wa Hatua wa Beijing;

Mtaalam wa Jinsia, Leticia Mkurasi, amesema Tanzania inashika nafasi ya 12 kati ya nchi zenye kiwango kikubwa cha ueneaji wa ukatili dhidi ya wanawake katika kanda ya Afrika.

Leticia amesema ukatili unaoripotiwa zaidi ni wa kimwili, kisaikolojia, kingono na kiuchumi na kwamba unazidi kuongezeka na kutokea katika mikoa mingi. 

Aliyekuwa Mbunge wa kwanza mwanamke kuchaguliwa mwaka 1985, Shamim Khan Jimbo la Morogoro Mjini akizungumza kwenye maadhimisho ya siku ya wanawake duniani yaliyoandaliwa na Mtandao wa Jinsia Tanzania( TGNP) jijini Dar es Salaam
Hata hivyo, amesema ukatili mwingi unafanyika nyumbani, alifafanua kuwa ukatili wa wapenzi wa karibu ndio aina inayoongoza, kwani kiwango kilichoripotiwa cha ukatili miongoni mwa wanawake walioolewa nchini Tanzania ni asilimia 78 katika mikoa ya Mara na Shinyanga. 

Ameongeza kuwa, kuanzia mwaka 2019 hadi 2021, kuliripotiwa matukio 79 ya mauaji ya wapenzi (IPV), wengi wao walichochewa na wivu. 

Akirejea ripoti ya 2023 kutoka kwa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), amesema inaonesha kuwa kati ya Januari na Septemba 2022, wanawake 472 waliuawa, sawa na wastani wa wanawake 53 kwa kila mwezi.

Pia, ripoti hiyo ilionyesha kuwa mwaka 2018, wanawake 544 waliuawa, mwaka 2019 walikuwa 437,  mwaka 2020 walikuwa 431 na mwaka 2024 walikuwa 554.

Mkurugenzi Mkazi wa UN Women nchini- Hodan Addou
Akizungumza katika maadhamisho hayo,  aliyekuwa Mbunge wa kwanza mwanamke wa kuchaguliwa nchini,  Shamim Khan, amepigilia msumari kuhusu ukomo wa wabunge wa vitimaalum, kwamba iwe ni miaka 10 tu, ili kutoa nafasi kwa wengine.

Shamim Khan, ambaye alichaguliwa kuwa Mbunge wa Morogoro Mjini mwaka 1985, amesema  uongozi ni chuo, hivyo ni muhimu  watu  kuhitimu, ili wengine wapate fursa, akiunga mkono kauli za viongozi kwamba ukomo wa wabunge na madiwani wa viti maalum uwe ni miaka 10.

Mtaalaam wa Masuala ya Jinsia Leticia Mkurasi akitoa wasilisho la tathmini ya hali ya ukatili wa kijinsia tangu maazimio ya Beijing
Katika hotuba yake, Shamim alikumbusha wanawake kujitokeza katika uchaguzi mkuu ujao kugombea nafasi mbalimbali za uongozi kwenye majimbo na kata, badala ya kutegemea nafasi za viti maalum. 

"Najivunia kuwa mwanamke wa kwanza nchini ambaye nilithubutu na kugombea ubunge na kushinda na baadaye kuwa Naibu Waziri wa Viwanda na Uwekezaji na Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto. 

Pia, nilianzisha mfumo wa wanawake kuwa na mabanda yao kwenye maonyesho ya Nane Nane," amesema  Shamim.

Mkurugenzi Mtendaji wa TGNP, Lilian Liundi, amesema  maadhimisho ya mwaka  2025, yanasherehekea utekelezaji wa Mpango Kazi wa Beijing baada ya miaka 30, huku akibainisha changamoto zinazowakabili wanawake na mikakati ya kuendeleza usawa wa jinsia na haki za wanawake.

"Hakika hatua kubwa imepigwa katika kupigania haki za wanawake na usawa, lakini bado kuna kazi kubwa mbele. Vituo vya taarifa na maarifa na serikali vinapaswa kuendelea kuhakikisha wanawake wanapata ulinzi na haki zao," amesema Lilian.

Wanaharakati: Juhudi kumkomboa mwanamke, ukatili kikwazo
Mkurugenzi Mkazi wa UN Women nchini, Hodan Addou, amekiri kuwa mafanikio yaliyopatikana katika kuongezeka kwa wanawake katika nafasi za uongozi, upatikanaji wa elimu na fursa za kiuchumi, huku mifumo ya sheria ikiwa imeboreshwa, ikiwemo sheria za uchaguzi, ili kuondoa vikwazo vinavyokwamisha haki za wanawake.

"Uwapo wa bajeti zinazozingatia mlengo wa kijinsia ni hatua muhimu. Mikakati inayotekelezwa ina lengo la kuhakikisha usawa wa kijinsia unakuzwa," ameongeza  Hodan.

Mratibu wa Agha Khan Foundation, Nelson Mhando, amesisitiza  kuwa miradi ya shirika hilo inajikita katika masuala ya usawa wa kijinsia, ikiwa ni pamoja na afya na elimu. 

Mtaalamu wa masuala ya Jinsia kutoka Mradi wa Maendeleo wa Umoja wa Mataifa (UNDP), Clara Maliwa, amesema  wanazidi kuondoa vikwazo vinavyowakabili wanawake katika kupigania usawa wa kijinsia, kuhakikisha uhuru na ushiriki wao katika jamii.