Barabara ya Somanga-Mtama yafungwa kwa muda

By Imani Nathaniel , Nipashe
Published at 04:11 PM Apr 06 2025
Barabara ya Somanga-Mtama yafungwa kwa muda
Picha: Mpigapicha Wetu
Barabara ya Somanga-Mtama yafungwa kwa muda

WAKALA ya Barabara Tanzania (TANROADS), Mkoa wa Lindi, imetangaza kusitisha matumizi ya barabara ya Somanga-Mtama, kwa muda baada ya mvua kubwa zilizonesha katika Wilaya ya Kilwa, mkoani Lindi.

Mvuoa hizo, zimeleta mafuriko makubwa yaliyoharibu eneo la barabara lililo kwenye njia ya mchepuko ya ujenzi wa daraja la Somanga-Mtama.

Meneja wa TANROADS Mkoa wa Lindi, Mhandisi Emil Zengo, amesema maji yamejaa katika eneo hilo na kusababisha barabara kutoweza kupitika kwa sasa.

Barabara ya Somanga-Mtama yafungwa kwa muda
"Kwa sasa tumeshamjulisha Mtendaji Mkuu wa TANROADS, Mhandisi Mohamed Besta na ametoa maelekezo kuhusu usalama wa watumiaji wa barabara, jambo ambalo ni muhimu kabisa. 

“Mtendaji Mkuu amelekeza barabara hii ifungwe, ili kutoa nafasi ya kuchunguza hali ya uharibifu na kuhakikisha usalama wa watumiaji wa barabara. Tunawashauri wananchi kuendelea kufuatilia taarifa zaidi kutoka mitandao ya kijamii ya TANROADS," alisema Mhandisi Zengo.

f645828a-0d57-41b1-a4c1-6f2967f1f2fb.jpg 73.56 KB
Ameongeza kuwa vifaa vya kazi vipo kwenye eneo la tukio na makandarasi wanaendelea na utekelezaji wa majukumu yao, ili kurekebisha hali hiyo haraka.

"Maji yatakapopungua, tutaanza kufanya kazi ya kurejesha mawasiliano na barabara itafunguliwa mara moja," ameongeza.

Mhandisi Zengo amesisitiza kuwa usalama wa watumiaji wa barabara ni kipaumbele cha kwanza, na hivyo kuwalazimu kuifunga barabara hiyo kwa muda. 

Amesema wananchi wataendelea kupewa taarifa rasmi kila hatua kuhusu maendeleo ya hali hiyo.