DC Mtatiro aipongeza DonBosco kuibua vipaji wanafunzi michezoni

By Marco Maduhu , Nipashe Jumapili
Published at 12:22 PM Mar 09 2025
Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga, Julius Mtatiro, akikabidhi kombe kwa washindi wa jumla katika mashindano ya michezo mbalimbali, kwa wanafunzi wa shule ya sekondari DonBosco
Picha: Marco Maduhu
Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga, Julius Mtatiro, akikabidhi kombe kwa washindi wa jumla katika mashindano ya michezo mbalimbali, kwa wanafunzi wa shule ya sekondari DonBosco

MKUU wa Wilaya ya Shinyanga, Julius Mtatiro, ameipongeza shule ya sekondari Don Bosco, iliyopo Didia wilayani Shinyanga, kwa kuendeleza utamaduni wa michezo shuleni, kwamba inasaidia kuibua, kukuza vipaji vya wanafunzi na kuimarisha afya zao.

Mtatiro amebainisha hayo, wakati alipokuwa mgeni rasmi katika uhitimishaji wa wiki ya michezo ya Don Bosco, akimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Anamringi Macha.

Akizungumza katika bonanza hilo, Mtatiro amesema michezo kwa wanafunzi ni muhimu kwa kuimarisha afya zao, kuibua vipaji, kuwajengea nidhamu, kupumzisha akili na hata kufanya vizuri kitaaluma.

Ameongeza kuwa michezo ni sehemu muhimu ya maisha ya kila mtu na wataalamu wa afya wanasisitiza umuhimu wa kufanya mazoezi, ili kuepukana na magonjwa nyemelezi.

DonBosco inavyoibua vipaji wanafunzi michezoni
“Hili jambo la michezo hapa Don Bosco nimelipenda. Utamaduni huu ni mzuri sana natamani hata kwa shule za serikali tuanzishe mashindano kama haya, ili kusaidia kuimarisha afya za wanafunzi, kuibua vipaji, kupumzisha akili zao na kujenga nidhamu,” amesema Mtatiro.

Pia, ametoa nasaha kwa wanafunzi, akiwashauri waendelee kushiriki michezo kuwa na nidhamu na kupenda masomo, ili waweze kutimiza ndoto zao na kuwa viongozi bora wa baadaye katika taifa hili.

Kwa upande wake, Mkuu wa Shule ya Sekondari Don Bosco, Padri Amani Meela, amesema kuwa shule hiyo inatambua umuhimu wa michezo na  kwamba michezo shuleni hapo, ni sehemu ya malezi ya watoto na inajenga nidhamu, kukuza ufanisi wa kitaaluma, kuboresha afya na kuibua vipaji.

1.jpg 131.41 KB
Padri Meela amefafanua kuwa wiki hiyo ya michezo ilianza Machi Mosi, 2025 na imehitimishwa Machi 8, mwaka huu, kwa michezo mbalimbali ikiwamo riadha, mbio za baiskeli, kuvuta kamba, sarakasi, pamoja na kuonyesha vipaji mbalimbali kupitia "houses" za shule, huku washindi wakipewa zawadi na vikombe vya ushindi.

Kaka Mkuu wa shule hiyo, Meshack Hunge, amesema michezo hiyo kwao inawajenga kiafya, kiakili, kuibua vipaji vyao, kuimarisha udugu, sababu katika michezo hiyo huwa wanaalika shule za jirani kushiriki na kufurahi pamoja.