Umuhimu wa Ushoroba wa Lobita-Dar kiuchumi

By Mwandishi Wetu , Nipashe
Published at 02:32 PM Mar 28 2025
news
Wizara ya Mambo ya Nje
Mkutano wa Mpango wa Mattei wa Afrika, Italia kuhusu Reli kuziunganisha Bahari za Atlantiki na Hindi

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mahmoud Thabit Kombo amependekeza Ushoroba wa Lobita kutoka Angola hadi Dar es Salaam upewe jina la Lobito – Dar, ili kusadifu uwezo wa reli ya kuunganisha Bahari za Atlantiki na Hindi.

Ushoroba huo unaunganisha nchi na nchi kuanzia Bahari ya Atlantiki kwa upande wa Angola hadi Bahari ya Hindi jijini Dar es Salaam.

Akizungumza Machi 27, 2025 katika Mkutano wa Mpango wa Mattei wa Afrika, Italia kuhusu Reli kuziunganisha Bahari za Atlantiki na Hindi, amesema mpango wa ushirikiano wa Maendeleo wa Italia na Afrika (Matttei Plan for Africa) unatarajiwa kuboresha miundombinu ya maendeleo Afrika kwa kuunganisha reli ya ushoroba huo.

Ushoroba wa Lobito umeunganishwa na miundombinu ya reli kwa nchi za Angola, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), na Zambia. 

Washiriki wa mkutano
Aidha, Mpango wa Mattei utasaidia kuboresha miundombinu ya maendeleo itakayoziunga nchi za Afrika na kurahisisha biashara na uwekezaji bila kusahau umuhimu wa Reli ya TAZARA.

Akizungumza katika mada kuu ya mkutano huo ya  uwekezaji katika miundombinu barani Afrika kupitia Ushoroba wa Lobito, Waziri Kombo ameipongeza Italia kwa mpango huu utaoibua fursa za kimkakati katika sekta za, biashara, uwekezaji, kilimo, madini pamoja na teknolojia  kwa kuiunganisha Bandari ya Dar es Salaam na Ushoroba wa Lobito.

“Tanzania ni tajiri wa ardhi yenye rutuba ambayo inaweza kuwanufaisha wafanyabiashara na wawekezaji wa Kiitaliano katika kilimo haswa kilimo cha kahawa. Uwekezaji utakaosaidia kupunguza changamoto zinazolikumba bara la Ulaya, ikiwemo uhamiaji haramu unaochochewa na ukosefu wa ajira kwa vijana wa Afrika,”amesema.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mahmoud Thabit Kombo
Naye, Waziri wa Uchukuzi wa Zambia, Frank Tayali, ameeleza maono ya serikali yao ya kubadilisha Zambia kutoka nchi isiyo na bahari hadi kuwa Taifa  kiunganishi ( land linked). Alisisitiza jukumu muhimu la Ushoroba wa Lobito na Reli ya TAZARA katika kuunganisha Zambia na majirani zake nane, kukuza ushirikiano wa kikanda, na kuwezesha biashara chini ya Eneo Huru la Biashara la Afrika.