"Rais Samia hadaiwi na wana Ubungo huduma ya maji" - Lukuvi

By Mwandishi Wetu , Nipashe
Published at 07:19 AM Sep 19 2024
Ziara ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu( Sera, Bunge na Uratibu) William Lukuvi Mradi wa Maji Mshikamano uliopo Kata ya Mbezi, Wilaya ya Ubungo.
Picha:Mpigapicha Wetu
Ziara ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu( Sera, Bunge na Uratibu) William Lukuvi Mradi wa Maji Mshikamano uliopo Kata ya Mbezi, Wilaya ya Ubungo.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu( Sera, Bunge na Uratibu) William Lukuvi ametembelea Mradi wa Maji Mshikamano uliopo Kata ya Mbezi, Wilaya ya Ubungo katika ziara yake ya kukagua miradi ya maendeleo katika Wilaya ya Ubungo ambapo amemshukuru na kumpongeza Rais Samia kwa kumaliza kwa kiasi kikubwa chagamoto ya huduma ya maji wilayani humo.

Waziri Lukuvi amesema Mradi wa Maji wa Mshikamano ni moja ya miradi ya kimkakati iliyolenga kuleta ahueni kwa wakazi wa Kata ya Mbezi ambao wamekua na changamoto ya maji kwa mda mrefu.

“Kwanza kabisa tunamshukuru Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan  kwa mradi huu wa Mshikamano kwa  kutoa fedha zaidi ya Bilioni 4.8 kwa ajili ya utekelezaji kwa wale wanayoifahamu Ubungo ya enzi hizo hali ya upatikanaji wa maji ulikua wa shida sana  lakini kupitia mradi huu wananchi wanapata nafuu, itoshe kusema Rais hadaiwi na wana Ubungo changamoto zipo haziwezi kukosekana  DAWASA ndo wakati wenu kuhakikisha mnazifanyia kazi Wananchi wapate maji” amesema Waziri Lukuvi

Naye Mkuu wa Wilaya ya Ubungo Hassan Bomboko amesema hali ya upatikanaji wa maji kwa wilaya ya Ubungo ni ya kuridhisha maeneo mengi na hayo ni matunda ya uwekezaji uliofanywa  na Serikali ya awamu ya sita na kwa maeneo machache ambayo huduma ya maji ina changamoto DAWASA wanatoa ushirikiano katika kuhakikisha changamoto zinafanyiwa kazi.

“Serikali ya awamu ya sita imefanya uwekezaji wa kutosha ndani ya miaka mitatu kwa upande wa sekta ya maji tunajivunja  utekelezaji wa mradi wa Mshikamano wananchi zaidi ya 200,000 wananufaika kupitia mradi huu, malalamiko yamepungua kwa hali ya juu kwa maeneo ambayo bado huduma haijatengemaa tunashirikiana na DAWASA kuhakikisha huduma inapatikana na kazi iliyobaki ni kufikisha huduma kwa wananchi zaidi” amesema Mhe. Bomboko

Naye Kaimu Afisa Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA) amesema Mradi wa Mshikamano ni moja ya miradi ya kimkakati iliyolenga kututatua changamoto ya maji kwa wakazi zaidi wa 200,000 wa Kata ya Mbezi, Mshikamano, Msakuzi, Mpiji- Magoe, Machimbo na Majengo mapya ambapo mradi umekamilika na unaendelea kutoa kutoa huduma kwa wanufaika.