DUCE yaja na mbinu kuachana na viboko, kazi ngumu shuleni

By Pilly Kigome , Nipashe Jumapili
Published at 03:46 PM Apr 13 2025
Naibu RAS Taaluma, Utafiti na Ushauri Elekezi (DUCE) Prof. Amani Lusekelo akizungumza na walimu waliopata mafunzo
Picha: Pilly Kigome
Naibu RAS Taaluma, Utafiti na Ushauri Elekezi (DUCE) Prof. Amani Lusekelo akizungumza na walimu waliopata mafunzo

CHUO Kikuu Shirikishi cha Elimu Dar es Salaam (DUCE), kimetoa mafunzo maalum kwa walimu 52 kutoka shule ya sekondari ya Mazoezi Chang’ombe kuwapa mbinu mpya mbadala, kutoa adhabu kwa wanafunzi bila athari na kuondoa adhabu kandamizi.

Mafunzo hayo wamepatiwa kupitia Kituo cha Utafiti kuhusu Ulinzi wa Mtoto na kuzuia Ukatili (CPVP) cha DUCE.

Naibu RAS Taaluma, Utafiti na Ushauri Elekezi (DUCE) Prof. Amani Lusekelo, amesema mafunzo hayo yamelenga kuwapa walimu mbinu mpya jinsi ya kutoa adhabu, kuepukana na adhabu kandamizi na kwenda kuwa mabalozi kwa shule zote nchini, kuwapatia mbinu hizo.

Naibu RAS DUCE Prof.Amani Lusekelo akimkabidhi cheti cha mmoja wa walimu waliopata mafunzo
Amesema utafiti wa kina uliofanyika umegundua adhabu kandamizi dhidi ya watoto husababisha msongo wa mawazo, matatizo ya akili, matatizo ya kisaikolojia na kusababisha kuzalisha idadi kubwa ya makatili katika jamii.

Amesema mbinu hizo mbadala zitakwenda kusaidia walimu kuepusha viboko visivyo na utaratibu, kuwabebesha mizigo mikubwa, kuwatukana wao na wazazi wao, kuwapa maneno ya kejeli, kuwadharau na kuwadhalilisha.

Naibu RAS DUCE Prof. Amani Lusekelo akimkabidhi cheti cha mmoja wa walimu waliopata mafunzo
Kupitia kituo hicho na utafiti wa kina uliofanyika wamegundua, kuna adhabu mbadala za kuwasaidia walimu kuwarekebisha tabia za wanafunzi pasipo kutumia adhabu kandamizi na mtoto akabadilika ikiwemo kujenga sekta ya elimu katika nchi .

Baadhi ya adhabu hizo mbadala, ikiwamo kumpa mwanafunzi adhabu ya kukaa kimya, ahadi, zawadi, kutengeneza urafiki naye, kumpa zawadi za mshtukizo (surprise), kama vile kumfanyia mambo apendayo kama kumpeleka ufukweni, itamfanya mtoto afikirie kwa kina, itamfanya afikirie zaidi mwalimu wangu anataka nini na itamfanya abadilike kitabia.

Walimu kutoka Shule ya Sekondari Mazoezi Chang'ombe wakimsikiliza mgeni rasmi mara baada ya mafunzo
Mhadhiri Mwandamizi na Mtiva Kituo cha Elimu (DUCE) Dk. Mabula Nkoba, amesema mafunzo hayo yana lengo la kuondoa adhabu kali zisizofaa dhidi ya wanafunzi na jamii kwa ujumla na kwenda kutengeneza taifa bora lisilo na athari sasa na kizazi cha baadae.

Amebainisha walimu hao wamesukwa, ili wawe kwenda kuwa mabalozi kwenda kutoa elimu kwa walimu wenzao na wazazi, kwenye shule zingine nchi nzima kuhusiana na mabadiliko ya adhabu shuleni.

“Elimu waliyoipata ni kubwa sana na wanakwenda kuwa mabalozi kwenda kutoa elimu kwa walimu wenzao na kuwapa mbinu kurekebisha mwanafnzi, bila kutumia adhabu kandamizi kwa kutumia maarifa waliyoyapata” amesema

Mhadhiri na Mratibu wa Kituo (CPVP), Dk. Faustine Bwire, amesema ziko njia nzuri sana za kumrekebisha mwanafunzi na kuzuia ukatili, ikiwamo kuwa na ukaribu na kumsikiliza mtoto kwa kina pindi anapokabiliwa na changamoto kutengeneza urafiki.

Pia, kuwashirikisha watoto kwenye mambo muhimu ya kifamilia hususani kumuelekeza mila, desturi na utamaduni pamoja na kuishi vyema na jamii iliyomzunguka.

Kutokupaza sauti kubwa kufoka pindi unapomuelekeza jambo fulani au kumpa katazo ya jambo hilo, na itamjengea urafiki na kumuelewa vizuri mwalimu au mzazi kwa haraka zaidi.

“Walezi na wazazi wengi wanakimbilia matusi na kumfokea kwa sauti mtoto na kumfananisha na wanyama kama vile kumuita mbwa, paka, nguruwe hiyo unazalisha tatizo kubwa la kumfanya huyo mtoto au mwanafunzi awe katili na kumuona adui mwalimu au mzazi na unazalisha vichocheo vya yeye aende kulipiza kwa watu wengine anapoanza kujitegemea,” amesema.

Mwalimu mnufaika wa mafunzo hayo, Tumaini Kasio, amesema wamepata faida kwenye mafunzo hayo na kupata suluhisho jinsi ya kuishi na wanafunzi na watoto na kuacha adhabu kandamizi na kutoa adhabu rafiki na kumbadilisha mwanafnzi.

“Unaingia nae mkataba mwanafunzi unamwambia ukifanikiwa kuacha tabia fulani basi nitakufanyia kitu fulani hapo unakuwa umeshammaliza na atabadilika kwa haraka zaidi,” amesema.