Mwili wa mwanaume mmoja anayekadiriwa kuwa na umri wa miaka 30 umekutwa ukiwa umelala ufukweni mwa Bahari ya Hindi, karibu na jengo la Mahakama ya Mwanzo Lindi, mapema asubuhi ya leo.
Kwa mujibu wa taarifa za Jeshi la Polisi mkoa wa Lindi, mwili huo uligunduliwa na mvuvi mmoja aliyekuwa akifanya shughuli zake katika eneo hilo. Uchunguzi wa awali umebaini kuwa marehemu hakuwa na majeraha yoyote yanayoashiria vurugu au shambulio, hivyo chanzo cha kifo chake bado hakijajulikana.
Hadi sasa, utambulisho wa marehemu haujafahamika. Mwili wake umehifadhiwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Lindi – Sokoine, ukisubiri uchunguzi wa daktari na ndugu kujitokeza kwa ajili ya utambuzi na taratibu nyingine zinazohitajika. Wakati huo huo, Jeshi la Polisi linaendelea na uchunguzi wa tukio hili ili kubaini kiini cha kifo hicho.
© 2025 IPPMEDIA.COM. ALL RIGHTS RESERVED