Lissu: Kuzuia uchaguzi si jambo jepesi

By Enock Charles , Nipashe Jumapili
Published at 02:16 PM Mar 30 2025
Wafuasi wa CHADEMA wakiwasikiliza viongozi wa chama hicho katika eneo la Vwawa wilayani Mbozi mkoani Songwe jana.
PICHA: MTANDAO
Wafuasi wa CHADEMA wakiwasikiliza viongozi wa chama hicho katika eneo la Vwawa wilayani Mbozi mkoani Songwe jana.

MWENYEKITI wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Tundu Lissu amesema kampeni ya chama hicho kuzuia uchaguzi usifanyike si jambo jepesi hivyo amewataka wanachama kujiandaa vyema.

Akizungumza na wanachama wa chama hicho wilayani Mbozi katika mkoa wa Songwe jana, Lissu alisema chama hicho ni cha kwanza tangu kuundwa kwa mfumo wa vyama vingi nchini kuja na mkakati wa kuzuia uchaguzi akisema kwamba halitakuwa jambo jepesi.

 “Tangu tumeingia mfumo wa vyama vingi vya siasa mwaka 1992, hakuna chama kimewahi kusema kwamba tusipokuwa na mabadiliko ya mfumo wa uchaguzi tutazuia uchaguzi sisi ni wa kwanza” alisema Lissu

 “Haya maneno ni makubwa, kuzuia uchaguzi maana yake ni kwamba ni kuzuia ratiba iliyowekwa kwenye sheria za uchaguzi na imewekwa kwenye Katiba ya nchi hii ya kufanya uchaguzi kila baada ya miaka mitano sisi tunataka kuizuia” 

 “Ni jambo dogo kiasi gani hili? wote wanafahamu ni jambo kubwa na hakuna ambaye amewahi kulisema katika miaka yote ambayo tumekuwa nchi ya vyama vingi” alisema Lissu.