Afisa Mifugo ahukumiwa kifungo kisa rushwa Missenyi

By Joctan Ngelly , Nipashe
Published at 06:35 PM Mar 24 2025
Afisa Mifugo ahukumiwa 
kifungo kisa rushwa 
Missenyi.
Picha: Mtandao
Afisa Mifugo ahukumiwa kifungo kisa rushwa Missenyi.

Mahakama ya Wilaya ya Missenyi, mkoani Kagera, imemhukumu Afisa Mifugo wa Kata ya Kanyigo, Eliezer Leonard Babu (35) kutumikia kifungo cha mwaka mmoja na mwezi mmoja jela kwa makosa mawili ya rushwa, ikiwemo kujipatia manufaa binafsi na kutowasilisha kiasi cha Sh milioni 2.58 za makusanyo ya tozo za Halmashauri ya Wilaya ya Missenyi.

Hukumu hiyo imetolewa na Hakimu Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Yohana Muyombo, baada ya upande wa mashtaka kuthibitisha makosa hayo pasipo kuacha shaka yoyote.

Hakimu Muyombo alisema mahakama imeamua kutoa adhabu kali ili iwe fundisho kwa mshtakiwa na kwa wafanyakazi wengine wenye tabia ya kujihusisha na vitendo vya rushwa.

Katika kesi hiyo, upande wa mashtaka ulikuwa ukiongozwa na mawakili wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Kagera, Kelvin Murusuri na Sospeter Joseph.

Mawakili hao waliwasilisha mashahidi sita na vielelezo nane, ambavyo vilithibitisha bila shaka kwamba mshtakiwa alihusika na makosa hayo.

Makosa Aliyoshtakiwa Nayo

  1. Kosa la kwanza: Mshtakiwa alishtakiwa kwa kosa la rushwa kwa kujipatia manufaa binafsi, kinyume na Kifungu cha 15(1)(a) na (2) cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa, Sura ya 329, marejeo ya mwaka 2022.
  2. Kosa la pili: Mshtakiwa alishtakiwa kwa kutotii wajibu wa kisheria, kinyume na Kifungu cha 123 cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu, ikisomwa pamoja na Sheria ya Serikali za Mitaa, Sura ya 290, kwa kushindwa kuwasilisha na kujinufaisha na makusanyo ya Sh milioni 2.58 za Halmashauri ya Wilaya ya Missenyi.