Vitongoji vinne vyapata maji safi na salama

By Shaban Njia , Nipashe
Published at 04:43 PM Mar 25 2025
Mbunge wa Ushetu, Emmanuel Cherehani (aliyevaa kimasai), akiziundua mradi huo wa maji leo, pembeni ni wakazi wa kijiji cha Mwadui.
Picha: Shaban Njia
Mbunge wa Ushetu, Emmanuel Cherehani (aliyevaa kimasai), akiziundua mradi huo wa maji leo, pembeni ni wakazi wa kijiji cha Mwadui.

WAKAZI 2,745 wa vitongoji vinne vya kijiji cha Mwadui, Kata ya Nyankende, Halmashauri ya Ushetu mkoani Shinyanga, vimepata huduma ya maji safi na salama.

Hatua hiyo inasaidia kuondokana na matumizi ya maji machafu yaliyokuwa yakisababisha watu kupata magonjwa ya kuhara na kuumwa matumbo.

Pia huduma hiyo, imewaondolea adha wanafunzi wa shule ya msingi Sinwankele, kutumia muda mwingi kutafuta maji ya matumizi ya msalani.

Kaimu Meneja wa RUWASA Wilaya ya Kahama, Mhandisi Paschal Mnyeti, ameyabainisha haya wakati wa uzinduzi wa upanuzi wa skimu ya maji Nyankende kwenda kijiji cha Mwadui, utakaohudumia vitongoji vinne vya Ilyamchele, Mwadui A, Igalula na Sinwankele.

Wakazi wa vitongoji hivyo wakifurahi upatikanaji wa huduma ya maji, leo
Amesema, mradi huo umetekelezwa na fedha za ufadhiri wa Usambazaji wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA), kupitia program ya lipa kwa matokeo (PforR), ujenzi wake ulianza Februari 7, mwaka jana na kukamilika Septemba 16, mwaka huo kwa gharama ya zaidi ya Sh. milioni 192,895.Mnyeti amesema, eneo la utoaji wa huduma utasimamiwa na kuendeshwa na chombo cha watoa huduma ya maji ya jamii (CBWSO) cha Mwanya na kitasimamia miradi ya maji iliyopo Kata ya Nyankende, Idahina, Ulewe na Ubagwe; mradi unatanki lenye ujazo wa lita 50,000 juu ya mnara wa mita 12.
Mbunge wa Ushetu, Emmanuel Cherehani, akizungumza na wakazi wa vitongoji vinne vya kijiji cha Mwadui wakati wa uzinduzi wa mradi huo
Miongoni mwa wakazi wa kijiji cha Mwadui, Salome Antony, amesema mradi umewasaidia kuondokana na matumizi ya maji ya kwenye madimbwi na visima walivyochimba kando ya mkazi yao, kwani ilisababisha kupata magonjwa ya kuumwa matumbo mara kwa mara.

“Watoto wetu walikuwa wanarudi kutoka shule wakiwa wamechoka sana na nikwasababu ya kutafuta maji, sasa hali hii wameondokana nayo baada ya kufikiwa na mradi wa majisafi na salama shuleni na wanasoma vema na imetuondoa hofu yao kutokufanya vema kwenye masomo,” ameongeza Antony.

Mbunge wa Ushetu, Emmanuel Cherehani, amesema serikali kupitia Wizara ya Maji, imeendelea kutatua changamoto ya ukosefu wa maji safi na salama katika maeneo ya pembezoni na kuwataka wananchi kutunza vyanzo vya maji na miradi yake, ili iendelee kuwanufaisha vizazi vyote.

Pia amesema, hivi karibuni walisaini mkataba wa upelekaji wa maji ya Ziwa Victoria kutoka Kahama-Ushetu, wenye gharama ya Sh. bilioni 44 na awamu ya kwanza utawafikia wananchi wa kata 11 na umetoa fursa za ajira zisizohitaji ujuzi kwa vijana wa kata husika.