Mama amuua mwanae kisha kumtupa shambani kwake

By Grace Mwakalinga , Nipashe
Published at 03:44 PM Dec 10 2025
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Benjamin Kuzaga

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya, linamshikilia Marry Timotheo, mkazi wa Garijembe kwa tuhuma za kumuua mtoto wake Scola Mwaba (10) , mwanafunzi wa darasa la nne katika Shule ya Msingi Ngonde.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa  Mbeya, Benjamin Kuzaga amethibitisha tukio hilo na kueleza kuwa limetokea Decemba 9,2025 majira ya saa 6:30 mchana eneo la Garijembe mtuhumiwa amuadhibu  mtoto wake kwa kumpiga kichwani na kitu kizito akimtuhumu kuwa ni mtukutu.


“Taarifa za awali za uchunguzi zinaeleza kuwa chanzo cha tukio ni kujichukulia  sheria mkononi ambapo baada ya kumpiga hadi kufariki dunia, Marry alimtupa  mwanae shambani jirani na  nyumba yake kwa msaada wa jirani yake Sharifa Nzalanje , ambaye naye anashikiliwa na Jeshi la Polisi kwa tuhuma za kushiriki kuficha kosa,” amesema Kuzaga.


Kamanda Kuzaga amesema upelelezi wa kesi hiyo unakamilishwa  kabla ya kuwafikisha watuhumiwa katika hatua zinazofuata za kisheria.

Ametoa wito kwa wazazi au walezi  kuepuka vitendo vya kujichukulia sheria mkononi kwa kutoa adhabu kali kwa watoto na badala yake kutumia mbinu za malezi na maadili zitakazosaidia  kuwalea bila kusababisha madhara kama vile vifo au ulemavu.