Jerry Silaa aagiza minara 758 kuwashwa ifikapo Mei 12

By Augusta Njoji , Nipashe
Published at 05:43 PM Mar 15 2025
Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari,  Jerry Silaa akizungumza na wananchi katika kijiji cha Kidete.
PICHA: MPIGAPICHA WETU
Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Jerry Silaa akizungumza na wananchi katika kijiji cha Kidete.

Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Jerry Silaa ameagiza kuwa ifikapo Mei 12, mwaka huu saa sita usiku, ujenzi wa minara ya mawasiliano vijijini uwe umekamilika na minara yote 758 iwe imewashwa, ili wananchi waweze kupata huduma za mawasiliano.

Waziri Silaa ametoa maelekezo hayo wakati wa ziara yake ya kukagua utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa minara 758 ya mawasiliano vijijini katika kijiji cha Kidete, Kata ya Chanzuru, Wilayani Kilosa, Mkoani Morogoro.

“Rais Samia ametenga kiasi cha fedha Sh. bilioni 126 kwa ajili ya ujenzi wa minara 758 ya mawasiliano vijijini, ambapo kukamilika kwake kutapunguza changamoto ya mawasiliano nchini,” amesema Waziri Silaa.

Ujenzi wa minara 758 ya mawasiliano vijijini unaotekelezwa na Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) unatarajiwa kunufaisha wananchi wapatao milioni 8.5 waishio vijijini.