Kamati ya bunge yafurahishwa ujenzi miundombinu ya reli nchini

By Mwandishi Wetu , Nipashe
Published at 03:11 PM Mar 14 2025
KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu
PICHA: MTANDAO
KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu

KAMATI ya kudumu ya Bunge ya Miundombinu imelipongeza Shirika la Reli Nchini (TRC) kwa usimamizi mzuri wa ujenzi wa reli ya kisasa (SGR), pamoja na maboresho ya miundombinu ya shirika hilo.

Kamati hiyo  imeitaka Mamlaka ya Bandari Nchini  (TPA) pamoja na shirika la Reli (TRC) kuanza kutekeleza mpango wake  wa  kuunganisha njia ya reli na bandari ya Tanga  ambapo kukamilika kwake kunatarajiwa kurahisisha usafirishaji wa ndani na nje ya nchi.

Mwenyekiti wa Kamati hiyo Suleiman Kakoso  alipofanya ziara ya kukagua na kutembelea miradi ya upanuzi wa bandari leo , uwanja wa ndege pamoja na maboresho ya reli ya mkoani hapa ameipongeza serikali kwa maboresho yanayofanyika katika miradi hiyo.

"Tumefurahishwa na mipango ya baadaye ambayo sasa mamlaka ya bandari inafikiria kwenda mbali zaidi muanze kuweka mifumo  ya kuunganisha  reli na bandari ili tuwe na miradi mikubwa"

Aidha ameipongeza serikali kupitia Wizara ya ujenzi na uchukuzi ambayo imeanza michakato ya ujenzi wa reli za kisasa katika maeneo mbalimbali nchini ambayo utakapo kamilika itafungua fursa mbalimbali ikiwemo za kiuchumi.

"Kitendo cha kuanza kufikiria kujenga reli za kisasa mikoani itasaidia sana kuongeza mzunguko wa fedha kwa wananchi wetu,tunashauri  serikali iwe inashirikisha wawekezaji  katika ujenzi wake" alisema Kakoso

"Pamoja na uwekezaji mkubwa ambao mnaweka kwenye shirika la reli, bunge linashauri ni vyema uwekezaji wenu uende sawa na  vitendea kazi ili uwekezaji uwe na tija" alisema.

Alisema mkoa wa Tanga unaendelea kufunguka kupitia fursa mbalimbali ikiwemo za kiuchumi katika utekelezaji wa miradi mikubwa kama  ujenzi wa barabara, ukarabati wa reli  sambamba na ujenzi wa barabara  ya Tanga hadi Singida pamoja na ile ya Tanga hadi Bagamoyo.

Kwa upande wake  Kaimu Mkurugenzi uendeshaji kutoka Shirika la Reli Tanzania (TRC) Focus Sahani ameeleza  kuwa  wameendelea kuhakikisha usafiri wa njia hiyo unaimarika ambapo hadi kufikia sasa kila wiki ya siku nne wanatoa huduma ya safari za treni za abiria kutoka Dar es salaam,Korogwe Moshi na  Arusha.

"Tumepata pongezi kubwa sana kuhusu uanzishwaji wa treni ya kisasa ya SGR pamoja  hiyo lakini tuna treni yetu ya MGR tunatoa huduma ya treni ya abiria katika mikoa ya Kanda ya Kaskazini kila wiki tuna safari nne za treni tangu tulipoifungua hiyo reli, kila  tunapofika kuanzia Mwezi Novemba mpaka Februari  huwa tunaongeza za treni zinakuwa  sita kwa wiki kwa ajili ya kuwahudumia watanzania" alisema  Sahani.