Mchungaji auawa kikatili na aliyefika kuombewa

By Mwandishi Wetu , Nipashe
Published at 01:56 PM Jul 01 2025
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mtwara, SACP Issa Suleiman.
Picha:Mtandao
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mtwara, SACP Issa Suleiman.

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mtwara linamshikilia Victor Fransis Thomas (39), mkulima na mkazi wa Kitongoji cha Kadudu, Kijiji cha Lupaso, Wilaya ya Masasi kwa tuhuma za mauaji ya kikatili dhidi ya Mchungaji wa Kanisa la Tanzania Assemblies of God (TAG), Thomas Rajabu Nkasimonga (58).

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mtwara, SACP Issa Suleiman, tukio hilo lilitokea Juni 27, mwaka huu, majira ya saa 12 jioni katika Mtaa wa Misheni, Kijiji cha Lupaso.

Kamanda Suleiman alisema kuwa siku ya tukio, mtuhumiwa alifika kanisani akiwa na baadhi ya ndugu zake kwa ajili ya kuombewa kutokana na matatizo ya kiafya yanayodaiwa kumkabili.

“Inadaiwa baada ya maombi ya muda mrefu, mtuhumiwa alionekana kuchoka, hivyo ndugu zake walimrejesha nyumbani kwa ajili ya kupumzika na kuendelea na maombi baadaye,” alisema Kamanda huyo.

Hata hivyo, hali ilibadilika ghafla baada ya kurudi nyumbani ambapo mtuhumiwa alitoroka kwa kutumia pikipiki na kurejea akiwa amebeba panga.

Alimvamia mchungaji huyo na kumshambulia kwa mapanga sehemu mbalimbali za mwili wake, na kusababisha kifo chake papo hapo kutokana na majeraha makubwa aliyoyapata.

Jeshi la Polisi linaendelea na uchunguzi wa kina kuhusu tukio hilo, na limeahidi kwamba mtuhumiwa atafikishwa mahakamani mara baada ya taratibu kukamilika.

Kamanda Suleiman ametoa wito kwa wananchi kuendelea kushirikiana na vyombo vya dola kwa kutoa taarifa zitakazosaidia kudhibiti matukio ya uhalifu katika jamii.