TIC yaendesha Kongamano la uwekezaji nchini Nigeria

By Joseph Mwendapole , Nipashe
Published at 09:05 PM Jun 12 2024
Mwenyekiti wa Bodi ya TIC, Dk. Binilith Mahenge.
Picha: Joseph Mwendapole
Mwenyekiti wa Bodi ya TIC, Dk. Binilith Mahenge.

SERIKALI ya Tanzania kwa kushirikiana na Ubalozi wa Nigeria imefanya kongamano kubwa la uwekezaji nchini humo lengo ikiwa ni kuvutia wawekezaji kutoka mataifa mbalimbali ndani ya Afrika.

Kongamano hilo ambalo lilifanyika kwenye miji ya Lagos na Enugu lililenga kuwaeleza wawekezaji wa Nigeria fursa mbaliambali za uwekezaji zinazopatikana hapa nchini.

Ujumbe wa Tanzania uliongozwa na Mwenyekititi wa Bodi ya Kituo cha Uwekezaji nchini (TIC), Dk. Binilith Mahenge.

Akizungumza kwenye kongamano hilo, Dk. Mahenge, alielezea mageuzi makubwa ambayo Rais wa awamu ya sita, Samia Suluhu Hassan ameyafanya na kuvutia uwekezaji kutoka nje.

Mmoja wa washiriki akizungumza kwenye kongamano hilo.
Alisema Tanzania imefanya mageuzi makubwa kwenye sheria na kanuni zinazosimamia uwekezaji na imeweka vivutio mbalimbali kwa wawekezaji wa ndani na wale wa kigeni.

“Katika kukuza diplomasia ya uchumi serikali ya Tanzania imefanikiwa kwa kiwango kikubwa kuboresha mazingira ya uwekezaji na biashara na hali hiyo imewavutia wawekezaji wengi kutoka mataifa mbalimbali,” alisema Dk. Mahenge

Washiriki wa kongamano hilo nchini Nigeria.
Kwenye kongamano hilo ujumbe wa Kituo cha Uwekezaji nchini (TIC) ulifanya vikao na wenzao wa Chemba ya Biashara na Viwanda Lagos na walikutana pia na Chemba ya Biashara, Viwanda, Madini na Kilimo  ya mji wa Enugu (ECCIMA).

Kongamano hilo lilijadili kuhusu sekta ya uzalishaji viwandani, ujenzi wa majengo, utalii, dawa, uchumi wa buluu, misitu, mifugo, huduma za kifedha, mafuta na gesi na uchakataji wa mazao ya chakula.

Washriki wakiwa kwenye picha ya pamoja.