Akamatwa tuhuma za ubakaji wa wanawake wanne

By Rehema Matowo , Nipashe
Published at 01:39 PM Oct 10 2025
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Gallus Hyera.
Picha: Mpigapicha Wetu
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Gallus Hyera.

Jeshi la Polisi mkoani Dodoma linamshikilia Piere Simon (20), kwa tuhuma za kubaka wanawake wanne katika mtaa wa Nzuguni B, jijini Dodoma.

Taarifa iliyotolewa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Gallus Hyera, na kuchapishwa kwenye ukurasa rasmi wa Jeshi la Polisi, imeeleza kuwa matukio hayo yanatuhumiwa kutokea Oktoba 5, 2025.

“Baada ya tukio hilo, polisi, wakishirikiana na wananchi wa eneo hilo, walifanikiwa kumkamata mtuhumiwa baada ya msako mkali,” amesema ACP Hyera.

Uchunguzi wa awali unaonyesha kwamba kijana huyo anaishi katika nyumba moja na watu wengine 13, jambo ambalo polisi wanasema linasaidia kuelewa mazingira yake.

ACP Hyera pia amebainisha kuwa mtuhumiwa atafikishwa mahakamani mara baada ya kukamilika kwa taratibu zote za kisheria.

Jeshi la Polisi limewataka wananchi kutojihusisha na kujichukulia sheria mkononi, bali kushirikiana na vyombo vya dola kwa kutoa taarifa za uhalifu ili hatua stahiki zichukuliwe.