Dk. Samia kufungua fursa za ajira Arusha ndani ya miaka mitano ijayo

By Romana Mallya , Nipashe
Published at 07:45 PM Oct 02 2025
Mgombea urais wa CCM, Samia Suluhu Hassan.
Pichs:Mpigapicha Wetu
Mgombea urais wa CCM, Samia Suluhu Hassan.

Mgombea urais wa CCM, Samia Suluhu Hassan, amesema ahadi zake kwa wananchi wa Arusha zinalenga kuwawezesha vijana na makundi mengine kujitegemea kiuchumi.

Akizungumza leo Oktoba 2, 2025 katika mkutano wa kampeni jijini Arusha, Samia ameahidi kufufua viwanda vilivyopo na kujenga kiwanda cha magadi soda Monduli. Pia amesema mashamba matano ya Kili Flora yaliyoshindikana kuendelezwa na wawekezaji yatatumika kuwapatia vijana kupitia Programu ya BBT ili kuwajengea fursa za kiuchumi.

Ameahidi kujenga mji wa Afcon City kuchochea utalii na kuongeza nafasi za ajira kwa vijana kupitia sekta hiyo. Vilevile, ameeleza kuwa serikali yake itahamasisha uwekezaji katika miradi ya kuongeza thamani ya madini ili kuongeza ajira.

Katika sekta ya utalii, Samia ameahidi kuvutia wawekezaji wakubwa kujenga hoteli za nyota tano na nne pamoja na kituo cha taarifa za utalii Arusha, hatua itakayoongeza nafasi za ajira na kipato kwa wananchi.