'Mimi, wewe na jamii, tukuze mazungumzo'

By Mwandishi Wetu , Nipashe
Published at 01:31 PM Jun 30 2025
Afya ya akili inaimarisha ustawi wa jamii
Picha: Mtandao
Afya ya akili inaimarisha ustawi wa jamii

TUREJESHE zama zile, jamii ya ushirika Ile jamii ya kale, ya simulizi hakika Tukae muundo ule, mambo kuzungumzika Mimi wewe na jamii, tukuze mazungumzo.

Tuzungumze uwazi, tusife tai shingoni 
Lipo jambo huliwezi, liseme usone soni 
Wapo wenye na ujuzi, wa jibu la mitihani 
Mimi wewe na jamii, tukuze mazungumzo

Pasiwe na wakubaki, kuyaficha maumivu 
Na machozi hayatoki, ishara mwenye nguvu ?
Kumbe lipo lipimiki, jambo lipo lilo bovu 
Mimi wewe na jamii, tukuze mazungumzo 

Tuseme yaliyo ndani, kuyaepusha madhara 
Jua umfwate nani, mtu mwenye na busara 
Awekaye kifuani, mtunzaji siri bora
Mimi wewe na jamii, tukuze mazungumzo. 

Uwepo mara kwa mara, muda wa mazungumzo 
Mazungumzo ni dira, na hutoa miongozo 
Huzipunguza hasara, nayo mengi matatizo
Mimi wewe na jamii, tukuze mazungumzo 

Jamii ijenge moja, nia kushirikiana 
Ifanane na daraja, la kuweza kuvushana 
Tukikaa kwa pamoja, kubwa huwa dogo sana 
Mimi wewe na jamii, tukuze mazungumzo 

Tuje afya ya akili, hili tupaze sauti 
Tusikwepe kujadili, hata kama hulipati 
Tulipe hadhi na hali, nia iwe madhubuti 
Mimi wewe na jamii, tukuze mazungumzo 

Mshairi: Dk. Raymond Nusura Mgeni, ni daktari wa afya na magonjwa ya akili. Kwa sasa anasomea masomo ya ubingwa eneo hilo katika Chuo Kikuu cha Sayansi na Tiba Shirikishi Muhimbili (MUHAS)