Watakiwa kutumia msimu wa mvua ipasavyo

By Julieth Mkireri , Nipashe
Published at 05:56 PM Apr 15 2025
Watakiwa kutumia msimu wa mvua ipasavyo
Picha: Julieth Mkireri
Watakiwa kutumia msimu wa mvua ipasavyo

WAKALA wa Huduma za Misitu (TFS) pamoja na Halmashauri za mkoa wa Pwani, zimetakiwa kutumia mvua zinazoendelea kunyesha hapa nchini kupanda miti katika maeneo ya mkoa huo kufikia lengo lililowekwa.

Maelekezo hayo yametolewa na Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, Shaibu Ndemanga, kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani, wakati wa uzinduzi wa siku ya upandaji miti katika Halmashauri ya Chalinze shule ya Msingi Chalinze Mzee ambapo miti 560 ilipandwa.

Amesema Mkoa huo unatakiwa kupanda miti milioni 13.5 kwa mwaka, kila halmashauri  itapanda miti milioni 1.5.

Pia amezitaka halmashauri kufuatilia miti inayopandwa iwe endelevu badala ya kutumia rasilimali nyingi kwenye upandaji miti ambayo haiendelei.

Watakiwa kutumia msimu wa mvua ipasavyo
"Uwiano wa miche inayopandwa na inayokuwa  hailingani fuatilieni hakikisheni miti inayopandwa inatunzwa kama tunapanda miti na hatuifuatilii kazi bure,” amesema.

Kamanda wa TFS Kanda ya Mashariki, PCO Mathew Ntilicha, akizungumza kwa niaba ya Kamishna wa Uhifadhi Prof. Dos Santos Silayo, amesema lengo la upandaji miti ni kuhamasisha jamii kuhifadhi misitu kwa manufaa ya sasa na vizazi vijavyo.

Watakiwa kutumia msimu wa mvua ipasavyo
Amesema maadhimisho hayo ya kupanda miti yanayofanyika Machi 21, kila mwaka, kwa 2025 yamebebwa na kaulimbiu: "Ongeza Thamani ya Mazao ya Misitu kwa Uendelevu wa Rasilimali za Misitu kwa Kizazi cha Sasa na Kijacho."

Ofisa Misitu Mkoa wa Pwani, Pierre Protas amesema pamoja na mchango mkubwa wa misitu kwa jamii, bado kuna changamoto zinazoikabili rasilimali hiyo ambazo ni pamoja na uanzishwaji wa mashamba na makazi.

Pierre ametaja changamoto nyingine kuwa ni utegemezi kwenye nishati ya kuni na mkaa kama chanzo cha nishati na kipato kwa jamii ndani na nje ya mkoa wa Pwani, pamoja na uhaba wa watumishi katika sekta ya maliasili.

Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Chalinze, ambaye pia ni Ofisa Elimu Msingi, Miriam Kihiyo naye amewaagiza walimu wakuu kuhakikishq kila mwanafunzi anapanda mti na kuitunza zaidi ya wanafunzi 61,000 huku akiomba TFS kuwasaidia dawa kwa ajili ya mchwa wanaohatibu miti.