NCCR Mageuzi yapitisha wagombea urais, makamu

By Mwandishi Wetu , Nipashe
Published at 11:44 PM Mar 29 2025
news
Mtandao
Mwenyekiti wa NCCR Mageuzi, Haji Ambar Khamis

CHAMA cha NCCR Mageuzi, kimewateua Ambar Khamis kupeperusha bendera ya urais huku mgombea mwenza akiwa ni Joseph Selasini katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba mwaka huu.

Wateule hao ambao ni Mwenyekiti wa NCCR Mageuzi Taifa, na Makamu Mwenyekiti,wamepitishwa Machi 29, mwaka huu katika mkutano mkuu uliofanyika jijini Dodoma na kuwaleta pamoja wanachama wa chama hicho.

Wakizungumza mara baada ya kuteuliwa waliahidi kufanya siasa za kistaarabu kw akulinda tunu za taifa ambazo ni amani, upendo na mshikamano.

Mwenyekiti wa NCCR Mageuzi, Haji Ambar Khamis, akizungumza mara baada ya kupitishwa kupeperusha bendera ya NCCR Mageuzi katika uchaguzi wa Oktoba 2025.
Aidha, wamekemea vitendo vya mmonyoka wa maadili pamoja na kushirikiana na vyama vyote vya siasa nchini kuhamasisha mageuzi na mabadiliko chanya katika jamii ikiwemo chama cha mapinduzi.

Kadhalika wameeleza kwamba watakuwa na sera ya kulinda na kutunza mazingira ili kudhibiti majanga ya mabadiliko ya tabia nchini ambayo yameendelea kuiathiri nchi yetu.

Wanachama wa NCCR Mageuzi wakiwa kwenye mkutano uliofanyika Dodoma Machi 29,2025
Aidha, chama hicho kimesema kitatoa ushirikiano wote kwenye uchaguzi mkuu wa Oktoba mwaka huu ambao utachagua rais, wabunge na madiwani.

Hadi sasa kati ya vyama 19 vyenye usajili wa kudumu vilivyotangaza na kupitisha wagombea urais wao ni CCM ambao kwenye mkutano maalum mwezi Januari, 2025 walimpitisha Rais Samia Suluhu Hassan kuendelea kutetea nafasi ya urais na Makamu wake ni Balozi Dk. Emmanuel Nchimbi.

Aidha, Rais Hussein Ali Mwinyi alipitishwa kuendelea kutetea nafasi hiyo kwa upande wa Zanzibar.

Machi 20, mwaka huu, Katibu Mkuu wa NLD, Hassan Doyo alitangaza kuwania urais na kuchukua fomu ndani ya chama chake huku akitaja vipaumbele 10 iwapo atapewa ridhaa na watanzania kushika wadhifa huo.