TIMU ya Polisi Tanzania, itatumia Uwanja wa Tanzanite Kwaraa, uliopo Babati mkoani Manyara katika mechi yake dhidi ya Geita Gold katika Ligi ya Championship Jumamosi hii.
Akizungumza na waandishi wa habari, Ofisa Habari wa Kikosi cha Polisi Tanzania, Inspekta Frank Lukwaro, amesema wameamua kutumia uwanja huo, baada ya uwanja wa Ushirika-Moshi, kuwa katika matengenezo.
Amesema Polisi Tanzania ni ya Watanzania wote hivyo hata Manyara ni nyumbani kwa timu hiyo, hivyo wakazi wa babati wajitokeze kwa wingi kufurahia burudani.
"Sisi kila Mkoa ni wenyeji hivyo hatuna shaka na wakazi wa Babati wameonesha kufurahia ujio wetu na wameahidi kutupa ushirikiano," amesema Lukwaro.
Amefafanua kuwa kwa sasa maandalizi kuelekea mchezo huo, yanaendelea vyema na wanaamini wataibuka na ushindi.
Timu ya Polisi, ipo nafasi ya 10 ikiwa na alama 24, baada ya kucheza mechi 21.
© 2025 IPPMEDIA.COM. ALL RIGHTS RESERVED