Mgombea urais wa Zanzibar kupitia CCM, Dk. Hussein Ali Mwinyi, amewahakikishia wananchi kuwa Serikali itaendelea kutekeleza miradi ya maendeleo kwa usawa kati ya Unguja na Pemba.
Akizungumza na wafanyabiashara wa soko la Chakechake, Mkoa wa Kusini Pemba, Dk. Mwinyi amesema Serikali itaendeleza sekta za miundombinu, elimu, afya na uwezeshaji kiuchumi bila upendeleo.
Amesisitiza kuwa soko la asili la Chakechake litalindwa ili libakie na uasili wake, huku likiimarishwa kwa ujenzi wa soko jipya la kisasa.
Kuhusu uwezeshaji, ameahidi kuongeza mara dufu fedha za mikopo kwa wajasiriamali na kushughulikia changamoto za msururu wa kodi kwa kuandaa mfumo nafuu kwa wafanyabiashara.
Dk. Mwinyi amewaomba wananchi kumpa ridhaa kupitia kura ili aendelee kuwaletea maendeleo zaidi.
© 2025 IPPMEDIA.COM. ALL RIGHTS RESERVED