Ni zamu ya Singida, mgombea urais CCM kunadi sera na Ilani

By Thobias Mwanakatwe , Nipashe
Published at 11:36 AM Sep 08 2025
Mgombea urais kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk. Samia Suluhu Hassan.
Picha: Mpigapicha Wetu
Mgombea urais kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk. Samia Suluhu Hassan.

Mgombea urais kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk. Samia Suluhu Hassan, kesho (Jumanne) anatarajia kuanza ziara ya siku mbili mkoani Singida kwa ajili ya kunadi sera na ilani ya chama hicho.

Katibu wa Siasa na Uenezi Mkoa wa Singida, Elphas Lwanji, akizungumza na waandishi wa habari leo (Septemba 8, 2025) amesema Dk.Samia atapokelewa katika Wilaya ya Manyoni na kufanya mkutano wa kampeni kuzungumza na wananchi kwenye viwanja vya soko la kuku.

Amesema mkutano wa pili utafanyika Wilayani Ikungi kwenye viwanja vya stendi na baadaye mchana kutafanyika mkutano mkubwa kwenye viwanja vya Bombadia vilivyopo Manispaa ya Singida.

Lwanji amesema siku ya pili (Jumatano) mgombea urais CCM Dk.Samia ataendelea na ziara ambapo atafanya mkutano kwenye uwanja wa Lulumba wilayani Iramba na hivyo kukamilisha ziara yake mkoani Singida

Lwanji amewaomba wananchi kujitokeza kwa wingi kumpokea Dk. Samia  ambapo atatumia mikutano hiyo kunadi sera na ilani ya chama kwa wananchi na kuelezea mafanikio makubwa ya maendeleo aliyofanya na serikali katika sekta mbalimbali zikiwamo afya, elimu, barabara na kilimo.

Katibu wa Siasa na Uenezi Mkoa wa Singida, Elphas Lwanji.