Mgombea wa urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk. Samia Suluhu Hassan, leo ameendelea kuinadi Ilani ya chama hicho kuelekea Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, huku akitangaza mpango wa kujenga reli mpya ya kisasa kutoka Tanga, Arusha hadi Musoma endapo wananchi watampa ridhaa ya kuongoza tena.
Akihutubia wananchi mjini Tanga, Rais Samia amesema utekelezaji wa mradi huo wa reli ya kisasa, yenye urefu wa takribani kilomita 1,108, utaanza mara tu baada ya uchaguzi. Reli hiyo itaanzia Bandari ya Tanga, kupita Arusha na kuishia Musoma.
Rais Samia amebainisha kuwa mradi huo utafungua maeneo ya viwanda na madini, jambo litakaloongeza ajira na kukuza fursa za kiuchumi kwa Mkoa wa Tanga na kanda nzima ya kaskazini.
“Reli hiyo ya kisasa ni sehemu ya mpango wa maboresho ya Bandari ya Tanga kuwa eneo maalum la bohari ya mafuta na gesi,” amesisitiza Rais Samia.
© 2025 IPPMEDIA.COM. ALL RIGHTS RESERVED