TIMU ya KMC inatarajia kucheza mchezo wa kirafiki mwishoni mwa wiki hii, dhidi ya KMKM ya Zanzibar, ikiwa ni mchezo wao wa kwanza tangu waanze kambi yao, visiwani humo.
Akizungumza na Nipashe jana, Msemaji wa timu hiyo, Khalid Chukuchuku, alisema lengo ni kucheza michezo mingi ya kirafiki kwa ajili ya kuangalia uwezo wa kila mchezaji.
"Jumapili tunatarajia kucheza mchezo wetu wa kwanza wa kirafiki ambao utamsaidia kocha wetu kuona uwezo wa wachezaji wake wote," alisema Chukuchuku.
Alisema tangu waanze kambi hiyo, wachezaji wote wanaendelea vizuri na kwamba hawana majeruhi katika kikosi chao.
Aidha, alisema wachezaji wamefurahishwa na ujio wa Kocha mpya, Marcio Maximo, ambaye alitambulisha kwao siku chache zilizopita.
Aliwataka mashabiki pamoja na wadau wa mpira Wilaya ya Kinondoni, kuendelea kuiunga mkono timu yao ili ipate matokeo mazuri msimu mpya utakapoanza kutimua vumbi mapema mwezi ujao.
Alisema lengo lao ni kushika nafasi ya juu kwenye msimamo wa Ligi Kuu msimu ujao kwa kufanya vizuri katika michezo yao yote.
© 2025 IPPMEDIA.COM. ALL RIGHTS RESERVED