Ukraine imeendeleza mashambulizi yake ya kimfumo dhidi ya sekta ya mafuta ya Urusi ikilenga kiwanda cha kusafisha mafuta katika eneo la kusini, haya ni kwa mujibu wa mamlaka ya Urusi wakati ambapo inasubiri silaha zaidi kutoka kwa washirika wake ikiwamo Marekani.
Mamlaka hiyo ya Urusi katika eneo la Krasnodar, imeripoti kuzuka kwa moto mdogo kwenye kiwanda cha kusafisha mafuta cha Afipski na kusema sehemu za droni moja ziliangukia kiwanda hicho.
Hata hivyo wamesema hakukuwa na majeruhi. Kulingana na vyanzo kutoka Ukraine, kiwanda hicho kinachozalisha petroli na dizeli, awali kilishambuliwa mnamo Agosti 28.
Wataalamu wanakadiria kuwa Urusi imepoteza takriban robo ya uwezo wake wa usindikaji kutokana na mashambulizi ya mara kwa mara dhidi ya viwanda vya kusafisha mafuta, vituo vya mafuta na vya upakiaji. Hali hii imesababisha uhaba wa dizeli na petroli katika baadhi ya mikoa.
Chanzo: dw
© 2025 IPPMEDIA.COM. ALL RIGHTS RESERVED