Biteko: Tanzania ina umeme wa kutosha

By Mwandishi Wetu , Nipashe
Published at 05:45 PM Jul 10 2025
Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko akikagua mitambo
mbalimbali ya umeme wa Gesi mara baada ya kutembelea Kituo cha kuzalisha umeme
cha Kinyerezi Julai 10, 2025 jijini Dar es Salaam
Picha: ONWM & WN)
Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko akikagua mitambo mbalimbali ya umeme wa Gesi mara baada ya kutembelea Kituo cha kuzalisha umeme cha Kinyerezi Julai 10, 2025 jijini Dar es Salaam

NAIBU Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dk. Doto Biteko, amesema Tanzania ina umeme wa kutosha baada ya kukamilika kwa miradi mikubwa ya uzalishaji umeme, ukiwamo Mradi wa Bwawa la Julius Nyerere (JNHPP ), ambao pekee unazalisha Megawati 2,115.

Naibu Waziri Mkuu ameyasema hayo leo, Julai 10, 2025, wakati wa ziara yake ya kukagua ya miradi ya kuzalisha umeme, kwa kutumia gesi asilia ya Kinyerezi I, Kinyerezi I Extension na Kinyerezi II, jijini Dar es Salaam.

Amesema licha ya kazi kubwa inayofanywa na TANESCO,  baadhi ya maeneo yalikabiliwa changamoto ya upatikanaji wa umeme lakini mpaka sasa yameendelea kuimarika.

Biteko amefafanua kuwa upatikanaji wa umeme unaendana na mahitaji ya ongezeko la watu na TANESCO, inatarajia kuongeza uzalishaji umeme  katika Kituo cha Kinyerezi III kutoka megawati 600 katika mpango wa awali hadi kufika Megawati 1,000.

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko akitembelea Kituo cha kuzalisha umeme cha Kinyerezi Julai 10, 2025 jijini Dar es Salaam
‘’Nataka niseme mbele yenu ndugu zangu, Rais Samia ndio kinara wa kufanya haya yote yafanikiwe amefanya uwekezaji mkubwa kwenye sekta ya nishati na ndio maana kwenye bajeti iliyopita wizara hii imepata Sh. trilioni 2.3 kikubwa anataka wananchi wapate umeme wa uhakika,’’ amesema Dk. Biteko.

Aidha, Naibu Waziri Mkuu pia ametumia nafasi hiyo kuipongeza TANESCO kwa maboresho makubwa yanayoendelea kufanyika ya kuwahudumia wateja hasa kwa uharaka wao wa kukabiliana na dharula zozote za umeme zinazojitokeza.

“Kuna maboresho makubwa yamefanyika katika kuwahudumia wananchi naona jitihada kubwa zinafanyika, mmekuwa na uharaka wa kushughulikia changamoto  za umeme lakini pia niwapongeze kwa kuimarisha kituo cha miito ya simu sasa wananchi wanahudumiwa bila gharama yoyote,’’ amesisitiza Dk. Biteko.

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko akishuhudia uzalishaji wa umeme kupitia vifaa maalum vinavyoonesha uzalishaji huo mara baada ya kutembelea Kituo cha kuzalisha umeme cha Kinyerezi Julai 10, 2025 jijini Dar es Salaam
Vilevile, Dk. Biteko ametembelea Kituo cha Kupokea Gesi Asilia Kinyerezi, kwa ajili ya kukagua miundombinu ya kusafirisha gesi na kuwataka kuongeza uzalishaji wa gesi, ili kusaidia kukidhi ongezeko la mahitaji ya umeme.

Katika ziara hiyo Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dk. Doto Biteko, ameongozana na viongozi mbalimbali, akiwamo Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mha. Felchesmi Mramba, Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo na  Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO Lazaro Twange.