WAZIRI wa Katiba na Sheria, Dk. Damas Ndumbaro, kesho anatarajiwa kuendesha kliniki ya utatuzi wa migogoro kwa Wananchi katika Banda la Wizara hiyo kwenye maonesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam(DITF).
Kwa mujibu wa Mkurugenzi Msaidizi wa Wizara hiyo, Beatrice Mtembo, Waziri atakuwa anasikiliza na kutatua migogoro inayogusa maeneo mbalimbali ikiwamo ardhi, mirathi, ndoa na mingine ya kijamii.
Amewaomba wananchi kujitokeza kwa wingi katika banda hilo ili kuhudumiwa kwenye matatizo yao mbalimbali yanayowakabili.
"Hii ni fursa ya kipekee kwa sababu, Waziri atasikiliza na kutatua migogoro ya wananchi papo hapo, kwa hiyo wasiikose fursa hiyo," amesema Beatrice.
Amesema lengo lao ni kuhakikisha kwamba kila mwananchi atakayefika katika banda hilo anatatuliwa tatizo lake kwa uharaka.
© 2025 IPPMEDIA.COM. ALL RIGHTS RESERVED