Wizara ya Maji kwa kushirikiana na Chemba ya Migodi Tanzania pamoja na watalaam wa Kampuni ya Uhandisi ya City wameshirikiana kuandaa mafunzo ya siku tatu (3) yatakayoshirikisha wataalam kutoka Sekta Binafsi na Serikalini ikiwamo wamiliki wa migodi kwa ajili ya usalama wa mabwawa ya majisafi na tope sumu (TSF).
Mafunzo yatafanyika jijini Mwanza kuanzia Novemba 19-21, 2025 yakiwa na kaulimbiu isemayo ‘Tahadhari za dharura za Kukabiliana na Majanga ya Mabwawa ya Maji na Tope sumu’ .
Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Maji, Diana Kimario ambaye pia ni Mkurugenzi Tathmini na Ufuatiliaji akiongea na vyombo vya habari Mtumba jijini Dodoma amesema mafunzo hayo hufanyika kila mwaka na mwaka 2025 ni mara ya tatu mfululizo ambapo mafunzo yamekuwa na mchango chanya katika kujenga uelewa wa namna bora ya kukabiliana na matatizo yanayotokana na mabwawa yakiwemo mabwawa ya tope sumu.
Aidha mafunzo hayo yamekuwa yakijumuisha wataalam waliobobea kutoka mataifa yaliyoendelea kwenye eneo linalohusu usalama wa mabwawa jambo ambalo limewezesha ufanisi wa mabwawa na kuepusha changamoto zinazosababishwa na mabwawa.
Amesisitiza kuwa Serikali chini ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan inaamini katika ushirikishwaji wa wadau wa sekta binafsi hivyo Wizara ya Maji itaendelea kuwa karibu na wadau hao ili kuhakikisha malengo yanafikiwa.
Amewataka wadau wote wa mabwawa ndani na nje ya nchi kujitokeza kujiandikisha ili kushiriki mafunzo hayo.
Mtendaji Mkuu wa Chemba ya Migodi Tanzania (Tanzania Chamber of Mines-TCM) Benjamini Mchwampaka ameipongeza serikali kwa jinsi ambavyo imekuwa ikitoa ushirikiano katika utekelezaji wa majukumu. Amesema wataendeela kuwa pamoja ili kuhakikisha sekta ya maji na madini kwa ujumla zinakuwa na kuifikia jamii.
© 2025 IPPMEDIA.COM. ALL RIGHTS RESERVED