Samia, Nchimbi wachukua fomu kugombea urais

By Renatha Msungu , Nipashe
Published at 12:52 PM Aug 09 2025
news
Picha Ibrahim Joseph
Mgombea urais CCM Samia Suluhu Hassan na mgombea mwenza Balozi Dk. Emmanuel Nchimbi baada ya kuchukua fomu ya kuomba ridhaa ya kugombea nafasi hiyo.

MGOMBEA urais kwa tiketi ya Chama cha Mapinduzi (CCM) Samia Suluhu Hassan pamoja na mgombea mwenza Balozi Dk. Emmanuel Nchimbi wamefika katika Ofisi za Tume Huru ya Uchaguzi (INEC) na kuchukua fomu ya kuomba ridhaa ya kugombea nafasi hiyo.

Uchukuaji fomu huo umefanyika leo mkoani Dodoma, ambako pia wananchi mbalimbali makada wa chama hicho wamejitokeza kwa wingi katika viwanja vya Makao Makuu ya CCM, wakimsubiri Mgombea Urais Samia, pamoja na mgombea mwenza Balozi Dk. Nchimbi, kwa ajili ya kuzungumza na wanachama na wafuasi wa chama hicho.

Wananchi hao wameonekana wamejaa barabarani wakiwa wameshika mabango yenye jumbe mbalimbali ikiwemo 'Oktoba tunakiti' huku wakisubiri kwa hamu msafara wa wagombea hao kutoka Ofisi za Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), zilizopo Njedengwa.

1
Husna Suleiman, mmoja wa wananchi waliokuwepo katika eneo hilo, amesema wamejitokeza kwa lengo la kuonyesha mshikamano wao kwa Samia na kumuunga mkono katika safari yake ya kuwania muhula mwingine wa urais. "Tuko pamoja naye na Oktoba tunaki," amesema.

Tukio hilo limepambwa na burudani kutoka kwa wasanii maarufu nchini, Mboso na Dulla Makabila, waliotumbuiza wakati wananchi na wanachama wa CCM wakiendelea kujumuika na kusubiri kuwasili kwa wagombea hao.