TUCTA: Kikokotoo kinatunyima usingizi

By Marco Maduhu , Nipashe
Published at 05:36 PM May 01 2025
Mratibu wa TUCTA Mkoa wa Shinyanga Ramadhani Pangara akizungumza kwenye maadhimisho siku ya Mei Mosi mkoani humo
Picha: Marco Maduhu
Mratibu wa TUCTA Mkoa wa Shinyanga Ramadhani Pangara akizungumza kwenye maadhimisho siku ya Mei Mosi mkoani humo

SHIRIKISHO la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA) Mkoa wa Shinyanga, limeiomba serikali kufanya marekebisho ya kikokoto na kurudisha cha awali cha asilimia 50.

Mratibu wa TUCTA mkoani Shinyanga, Ramadhani Pangara, amebainisha hayo leo Mei Mosi, 2025, wakati akisoma risala ya wafanyakazi mkoani humo, kwenye maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani.

"Tatizo la kikokotoo linatunyima usingizi, tunaomba serikali ilirudishe cha zamani cha asilimia 50 na siyo cha sasa kinatuumiza," amesema Pangara.

Siku ya Wafanyakazi Duniani
Ametaja changamoto nyingine ni wastaafu kutolipwa mafao yao kwa wakati na kuomba wanapomaliza likizo ya kwanza ni vyema wakapewa mafao yao.

Nyingine ni waajiri wa sekta binafsi kutozingatia sheria na taratibu za ajira na hata kutowapatia wafanyakazi wao mikataba ya kazi.

Alitaja nyingine, ni baadhi ya waajiri kutoruhusu wafanyakazi wao kujiunga na vyama vya wafanyakazi, na wanaotaka hupatiwa vitisho na hata wengine kufukuzwa kazi.

Siku ya Wafanyakazi Duniani
Nyingine ni kutopelekwa michango ya wafanyakazi wao kwa wakati kwenye mifuko ya hifadhi ya jamii kama NSSF, pamoja na kutowapatia hati za malipo.

Waliulalamikia pia Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya, kupunguza baadhi ya vifufurushi na kwamba ni kuwanyanyasa watumishi.

Pia, walilalamikia tatizo la baadhi ya waajiri, kutowapatia motisha wafanyakazi wao na hata kuwanyima zawadi katika Mei Mosi.

Siku ya Wafanyakazi Duniani
Aidha, ameiomba serikali iendelee kujali maslahi ya wafanyakazi, pamoja na kutatua changamoto ambazo zinawakabili, sababu wao ndiyo mhimili wa taifa.

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Anamringi Macha, amewataka wafanyakazi kuendelea kufanya kazi kwa bidii na weledi, wakati serikali ikiendelea kushughulikia changamoto ambazo zinawakabili.

Amesema serikali ilishatoa ajira mpya, watumishi kupandishwa madaraja na kwamba itaendelea kuboresha maslahi ya wafanyakazi.

Amesema kwa changamoto ambazo zimewasilishwa zote watazifanyia kazi, huku akimuagiza Katibu Tawala wa Mkoa huo, Salum Hamduni, kuunda timu ambayo watashirikiana na vyama vya wafanyakazi, ili kuitatua changamoto moja baada ya nyingine.

Katika hatua nyingine, amewataka wananchi pamoja na wafanyakazi, kwamba wajitokeze kwa wingi kuboresha taarifa zao kwenye Daftari la Kudumu la Wapigakura, ambalo tayari limeshaanza mkoani humo na litadumu kwa siku saba.