Wananchi waanzishiwa 'mwendo' upishi nishati safi

By Elizabeth Zaya , Nipashe
Published at 01:23 PM Jul 08 2025
Wananchi waanzishiwa 'mwendo' upishi nishati safi
Picha: Mtandao
Wananchi waanzishiwa 'mwendo' upishi nishati safi

SHIRIKA la Umeme Tanzania (TANESCO), limetoa zawadi ya majiko ya umeme kwa wananchi waliofika katika banda lao lililopo kwenye Maonesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa maarufu Sabasaba, ikiwa ni sehemu ya kuhamasisha matumizi ya nishati safi.

Akizungumza na waandishi wa habari jana katika viwanja vya maonesho hayo, Mkurugenzi Mtendaji  TANESCO, Lazaro Twange amesema wananchi waliofika katika banda lao wamepata fursa ya kupata elimu juu ya umuhimu wa matumizi ya nishati safi ya kupikia na kisha kupatiwa zawadi ya majiko ya umeme.

Amesema katika banda hilo, kuna majiko hayo ya umeme na wananchi waliojibu vema maswali waliyoulizwa wamepata fursa ya kujishindia zawadi ya majiko hayo, kwa ajili ya kuyatumia katika kupikia.

“Ni maelekezo ya Rais Samia Suluhu Hassan, kwamba watanzania tuhame kwenye kutumia nishati isiyokuwa safi na kutumia iliyosafi, hivyo hapa tunazungumzia nishati ya umeme na tuna majiko haya ya umeme yamefanyiwa utafiti na kuthibitika kuwa yanaweza kupikia na chakula kikaiva kwa kutumia chini ya Unit moja,

“Tunawashukuru watanzania kuja katika banda letu na kwa kuzingatia kuwa wanaelewa tumewashindanisha kwa maswali, aliyeshinda amepata zawadi ya jiko la Umeme, hivyo wakayatumie hayo majiko na wawe mabalozi wazuri kwa wengine,” amesema

Kaimu Meneja Mkuu wa Kampuni ya Ujenzi na Ukarabati wa Miundombinu ya Usafirishaji na Usambazaji wa Umeme (ETDCO), Sadock Mugendi, amesema wamekuwa wakisambaza na kusafirisha umeme maeneo mbalimbali vijijini na kwamba hivi karibuni wamemaliza mradi wa kusafirisha umeme kutoka Tabora mjini kuelekea Katavi wenye kilomita 383 na una msongo wa Kilovolt 132.

“Mradi huu ni mafanikio makubwa kwa Serikali hata hivyo tuna mradi mwingine Mbeya, Katavi yote tunasambaza umeme vijijini, tunaishukuru serikali kuendelea kutuamini kwa kutupatia miradi hii,” amesema

Meneja Mkuu Kampuni ya Uendelezaji Joto Ardhi Tanzania (TGDC), Mathew Mwangomba, amesema kwa sasa TGDC katika maeneo ya Mbeya wameanza kuhakiki rasilimali ya joto ardhi na kwamba umeme utakaopatikana utatumiwa katika matumizi ya moja kwa moja na matumizi yatakayoingizwa kwenye Gridi ya Taifa.

“Timu yetu ipo Mbeya eneo ya Mbozi na baada ya kufanya uhakiki tumebaini kuwa eneo hilo lina uwezo wa megawati 70 ambayo tutaingiza katika gridi ya Taifa, TGDC tunawaalika wadau wote wa ndani na nje kuja kuwekeza katika kampuni yetu,” amesema

Maonesho ya 49 ya Kimataifa ya Dar es Salaama, yalianza rasmi Juni 28 na yanatarajiwa kufungwa Julai 13.