Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amesema serikali yake imejipanga kupunguza gharama za vifaa vya ujenzi ili kuwawezesha wananchi kumudu ujenzi wa makazi bora na salama.
Akizungumza bungeni jijini Dodoma, Rais Samia amesema serikali itaweka mkazo maalum katika kuhakikisha Watanzania wanapata nyumba bora na nafuu, sambamba na kusimamia utekelezaji wa sera zinazolenga kuboresha hali ya makazi katika maeneo yenye mazingira duni.
“Tutaweka mkazo maalum kwenye nyumba bora na nafuu, na tutasimamia utekelezaji wa sera zinazolenga kuboresha hali ya makazi kwenye maeneo yenye makazi duni,” amesema.
Rais Samia amebainisha kuwa serikali itaendelea kushirikiana na sekta binafsi ili kuongeza uwekezaji katika miradi ya uendelezaji miji, ikiwemo ujenzi wa nyumba za gharama nafuu kwa wananchi wa kipato cha chini na kati.
“Sambamba na hilo, tutaongeza kasi ya urasimishaji wa maeneo ya makazi na kuimarisha utatuzi wa migogoro ya ardhi kwa kupima maeneo nchi nzima kwa kutumia teknolojia za kisasa,” ameongeza.
© 2025 IPPMEDIA.COM. ALL RIGHTS RESERVED