Kisabya wa NRA: Amani kwanza, huduma bure kwa Watanzania

By Adela Madyane , Nipashe
Published at 07:44 PM Sep 05 2025
Kisabya wa NRA: Amani kwanza, huduma bure kwa Watanzania
Picha: Mpigapicha Wetu
Kisabya wa NRA: Amani kwanza, huduma bure kwa Watanzania

Mgombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Chama cha National Reconstruction Alliance (NRA), Hassan Kisabya, amewahakikishia Watanzania kuwa amani itabaki kuwa nguzo kuu ya taifa endapo atachaguliwa kuwa Rais.

Akihutubia wakazi wa Buzebazeba, Manispaa ya Kigoma Ujiji, leo, Kisabya amesema usalama wa raia na kudumu kwa amani ndicho kipaumbele kikuu cha chama chake.

“Usalama wa watu ni jambo la msingi kuliko kitu kingine chochote. Ni amani ndio inatufanya tuwe hapa. Wanasiasa wachezee kila kitu ila wasichezee amani yetu. Mchukue kila mnachotaka ila amani yetu mtuachie,” amesema Kisabya.

Sera na Ahadi Kuu za NRA

Katika sera zake, Kisabya ameahidi:

  • Huduma za kijamii bure – ikiwemo matibabu, elimu, maji na umeme.

  • Matibabu bure kwa wananchi wote, isipokuwa huduma za anasa kama upasuaji wa kubadilisha maumbile au kuongeza muonekano wa mwili.

  • Kuweka walimu kwenye shule zote na vifaa tiba kwenye hospitali zilizopo, akisema serikali iliyopo tayari imeweka miundombinu, hivyo wao watazingatia uboreshaji.

  • Kukomesha wizi wa mtandao kwenye huduma za simu, hatua itakayofanikisha kulipa kila Mtanzania fidia ya GB 200 za intaneti mara baada ya kushinda.

Aidha, Kisabya amesisitiza kuwa serikali yake itapambana vikali na vitendo vya ushoga na usagaji, akieleza kuwa “maovu hayo hayana nafasi katika jamii ya Tanzania.”

Ushiriki wa Vijana

Kisabya amewataka vijana kuacha kususia uchaguzi na badala yake wajitokeze kupiga kura:

“Siasa ni chombo cha mabadiliko, na kila kura ina umuhimu mkubwa katika kuboresha maisha ya Watanzania. Vijana msipoteze nafasi hii,” amesisitiza.

Maoni ya Wananchi

Baada ya mkutano huo, Saida Ramadhani, mkazi wa Kigoma, amesema amefurahishwa na msimamo wa Kisabya kuhusu kulinda amani:

“Amani ndiyo nguzo ya maendeleo ya kila Mtanzania, sera zake zimetupa matumaini,” amesema.

Naye kijana Yusuph Omary amehimiza vijana kujitokeza kwenye mikutano na kusikiliza sera ili wafanye maamuzi sahihi siku ya kupiga kura.

Kampeni za NRA

Chama cha NRA kimekuwa cha kwanza kuzindua kampeni zake mkoani Kigoma na chama cha kumi kitaifa kuzindua kampeni tangu kuzinduliwa rasmi Agosti 28 mwaka huu.