Mwenge wa Uhuru waunga mkono hatua za RUWASA

By Marco Maduhu , Nipashe
Published at 04:01 PM Aug 05 2025
Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2025, Ismail Ali Ussi, akizundua mradi wa maji Halmshauri ya Ushetu.
Picha: Marco Maduhu
Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2025, Ismail Ali Ussi, akizundua mradi wa maji Halmshauri ya Ushetu.

KIONGOZI wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2025, Ismail Ali Ussi, amewapongeza Wakala wa Majisafi na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA), Mkoa wa Shinyanga, kwa utekelezaji wa miradi ya maji inayowanufaisha wananchi wa vijijini.

Ussi ametoa pongezi hizo jana Agosti 4, 2025, wakati wa uzinduzi wa mradi wa usambazaji maji katika vijiji vya Chona, Ubagwe na Bukomela vilivyopo katika Halmashauri ya Ushetu, wilayani Kahama.

1.jpg 45.3 KB
Amesema RUWASA imefanya kazi kubwa ya kuhakikisha wananchi wa vijijini wanapata huduma ya maji safi na salama, hatua ambayo imemuheshimisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, kwa kutekeleza kwa vitendo ahadi yake ya kupeleka huduma ya maji hadi vijijini.

"Rais Samia alivyoingia madarakani aliahidi kutekeleza miradi ya maji hadi vijijini. Leo tunaona utekelezaji huo kwa vitendo. RUWASA nawapongeza sana, mmemheshimisha Rais," amesema Ussi.

Aidha, amesema baada ya kukagua mradi huo kwa kina na kupitia nyaraka zake zote, wamejiridhisha kuwa umezingatia vigezo vyote vya utekelezaji na kwamba hauna dosari, hivyo Mwenge wa Uhuru umeridhia kuuzindua rasmi.

Amempongeza pia Meneja wa RUWASA Mkoa wa Shinyanga, Mhandisi Julieth Payovela na timu yake mgazi ya wilaya kwa kazi kubwa wanayoifanya kwa kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya maji.

Tangi la maji
Awali akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa mradi huo Meneja wa RUWASA wilaya ya Kahama Mhandisi Maduhu Magili, amesema vijiji hivyo vitatu vilikuwa na changamoto kubwa ya ukosefu wa maji kwa muda mrefu.

Amesema utekelezaji wa mradi huo ulianza Februari 14, 2024 na kukamilika Julai 28, 2025, ambapo chanzo cha maji ni visima virefu vitatu vilivyochimbwa katika vijiji husika kwa gharama ya Sh. bilioni 1.4.

Uzinduzi mradi wa maji
"Mradi unanufaisha jumla ya kaya 961 zenye wakazi wapatao 5,763 ambao sasa wanapata huduma ya maji safi na salama na Tayari wateja 21 wameunganishiwa huduma ya maji majumbani mwao," amesema Mhandisi Magili.

Kwa upande wao, baadhi ya wananchi wa Kijiji cha Bukomela, wamesema  mradi huo umewaondolea adha ya kutembea umbali mrefu kutafuta maji, na sasa wanatumia maji safi kwa shughuli za kila siku.