Serikali imesisitiza umuhimu wa huduma ya maji katika kukuza uchumi na maendeleo ya jamii nchini, ikibainisha juhudi zake katika kuhakikisha upatikanaji wa maji safi na salama kwa wananchi mijini na vijijini.
Akifungua Mkutano wa Mapitio ya Programu ya Sekta ya Maji jijini Dar es Salaam, Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi Zanzibar, Mhandisi Zena Said, amesema kuwa serikali imewekeza fedha nyingi katika sekta ya maji ili kuboresha huduma hiyo muhimu kwa wananchi.
Mhandisi Zena, akizungumza kwa niaba ya Katibu Mkuu Kiongozi, ameeleza kuwa serikali imepania kutimiza Lengo Namba Sita la Maendeleo Endelevu ya Umoja wa Mataifa (SDGs) linalohusu upatikanaji wa maji safi kwa wote.
Aidha, alisema serikali inashirikiana na wadau mbalimbali ili kuongeza nguvu katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi kwa kuhakikisha upatikanaji endelevu wa maji kwa jamii.
Amewataka washiriki wa mkutano huo kutoa maoni yao kuhusu mustakabali wa Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji, ambayo inatarajiwa kukamilika mwaka 2026.
Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, Mhandisi Mwajuma Waziri, amesema kuwa Wiki ya Maji ni jukwaa muhimu la kujadili changamoto zinazokabili sekta ya maji duniani na kutafuta suluhisho.
Ameeleza kuwa serikali imepanga kufanikisha upatikanaji wa maji kwa asilimia 85 vijijini na asilimia 95 mijini, huku ikihamasisha ushirikiano wa wadau mbalimbali ili kuhakikisha huduma ya maji inakuwa endelevu kwa maendeleo ya taifa.
© 2025 IPPMEDIA.COM. ALL RIGHTS RESERVED