Tanzania, Italia kuimarisha taasisi za elimu ya ufundi kupitia TELMS

By Grace Mwakalinga , Nipashe
Published at 12:25 PM Aug 06 2025
 Tanzania, Italia kuimarisha taasisi za elimu ya ufundi kupitia TELMS
Picha: Mpigapicha Wetu
Tanzania, Italia kuimarisha taasisi za elimu ya ufundi kupitia TELMS

Serikali kwa kushirikiana na nchi ya Italia kupitia Mradi wa TELMS II, wamekubaliana kuendeleza mageuzi ya Elimu ya Ufundi kwa kuziimarisha Taasisi za elimu ya ufundi ili kuchochea maendeleo nchini.

Katika kikao cha kamati ya pamoja kilichoketi Agosti 5,2025 kikiongozwa na Mwakilishi Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Elimu ya Juu, Dk. Kenneth Hosea kwa niaba ya Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia,  amesema  kiasi cha sh. bilioni 54  kitatumika kutekeleza mradi huo.

Amesema mradi huo wa miaka mitano unaoanza  2025/2030 utasaidia utekelezaji wa Sera ya Elimu na Mafunzo kwa sababu  unalenga kukuza teknolojia, ubunifu na ujasiriamali, pia utaimarisha maendeleo ya nishati endelevu pamoja na suala la uhifadhi mazingira.

Balozi wa Italia nchini Tanzania, Giuseppe Sean Coppola, amesema  wanajivunia mahusiano mazuri ya  kidiplomasia  kati yao, hasa kupitia ushirikiano katika miradi ya elimu inayolenga kuwajengea watanzania ujuzi na maarifa.

Mratibu wa Mradi huo, ambaye ni Mkurugenzi wa Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dk. Fredrick Salukele amewataja  wanufaika wa TELMS II kuwa ni Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia Mbeya (MUST), Chuo cha Ufundi Arusha (ATC), Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT) na Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Karume (KIST).

Viongozi mbalimbali wa vyuo hivyo walihudhuria kikao hicho wakiwamo Makamu Mkuu wa  MUST Prof. Aloys Mvuma, Mkuu wa ATC Prof. Musa Chacha, Mkuu wa DIT Prof. Preksedis Ndomba pamoja na  Mkuu wa Taasisi ya ya KIST Dk. Mahmoud Abdulwahab Alawi.