Askofu Kinyaiya: Tuwakumbuke wahitaji

By Beatrice Philemon , Nipashe
Published at 11:58 AM Dec 26 2025
Askofu Mkuu wa Jimbo kuu,  Katoliki la Dodoma, Mhashamu Beatus  Kinyaiya
PICHA: BEATRICE PHILEMON
Askofu Mkuu wa Jimbo kuu, Katoliki la Dodoma, Mhashamu Beatus Kinyaiya

Tunapoingia mwaka 2026, tutembee na Kristu, tumfanye awe jirani yetu, rafiki yetu, na tufanye sala katika maisha yetu ili atusaidie kutatua changamoto zinazotukabili katika maisha yetu.

Askofu Mkuu wa Jimbo kuu,  Katoliki la Dodoma, Mhashamu Beatus  Kinyaiya alisema hayo katika Misa ya mkesha wa kuzaliwa Bwana wetu Yesu Kristo iliyoadhimishwa usiku katika  Parokia ya  Mtakatifu Paulo wa Msalaba, Jimbo kuu la Dodoma.

Alisema mkifanya hivyo, mtaona vitu vilivyovigumu katika maisha yenu  vinapotea.  "Pia tunaposherekea sherehe ya kuzaliwa  mtoto Yesu, tunatakiwa tufanye kitu kwa wahitaji, jitahidi kutembelea wagonjwa, waone watoto yatima au katembelee magereza, wapelekee zawadi, unapofanya ukarimu kwa wahitaji , hawa masikini na wahitaji ni chombo cha kupata neema kwako, " alisema   

Aliomba  waumini waliohudhuria ibada hiyo  kubeba msalaba wao pamoja na Yesu watapata faraja kwa sababu Yesu pia  alipata taabu  zote kama wanazozipitia katika maisha yao. "Tumtegemee atatusaidia kutatua changamoto zetu, tuwe  na imani atatusaidia, tusimuache, watu wengine wanaamua kujinyonga kwa sababu hawana imani na Yesu," alisema 

Alitaja taabu alizopitia Yesu  kuwa ni, Yesu  alizaliwa kwenye zizi la Ng'ombe sehemu yenye harufu mbaya, amezaliwa  familia yenye kipato cha chini, hata kijiji alipozaliwa ni pembeni, siyo kwenye Kasiri ya Kifalme, alisema.

" Nimejiuliza kwanini Mungu alitaka Yesu azaliwe hivyo? alitaka tujifananishe naye, kila mtu ana changamoto zake katika maisha, mwingine  anachangamoto kazini, majungu, kijicho, wengine wana changamoto  katika ndoa, mtu   anagombana na mama mkwe, mawifi, wengine wanasubiri kuolewa bwana haji, wengine sikukuu imefika hawana hela, watu wanapesa zao lakini  hawataki kulipa, " alisema. 

Alisema, sasa hivi  pia Kuna mabadiliko ya tabia nchi,  tunapata joto sana, na mwaka 2026 utakuwa siyo mzuri, huyu mtoto Yesu aliyezaliwa atupe faraja katika yale yote tunayopitia, alisema.  Aliomba akina baba kukaa nyumbani kwao," ukae nyumbani watoto wakuone, utaenda kutembea kwa rafiki zako siku nyingine,  hii  ni siku ya familia.

Mbali na hilo alishukuru waumini kumpa zawadi ya Noeli, na kuwambia Mwenyezi Mungu akafanye maajabu katika maisha yao, na awaongezee walipotoa. Misa hiyo iliadhimishwa kwa kushirikiana na  Padri Beno Mganga, Paroko wa Parokia ya Mtakatifu Paulo wa Msalaba na Padri Saimon Swaga, Wakili Paroko wa Kanisa hilo.