Askofu Ndizeye: Tupende kujifunza kuhusu imani yetu

By Beatrice Philemon , Nipashe
Published at 04:20 PM Dec 26 2025
Askofu wa Jimbo Katoliki Kahama, Mhashamu Christopher Ndizeye
PICHA: MPIGAPICHA WETU
Askofu wa Jimbo Katoliki Kahama, Mhashamu Christopher Ndizeye

Askofu wa Jimbo Katoliki Kahama, Mhashamu Christopher Ndizeye amewashauri waumini kuchangamkia fursa za mafundisho ya dini wanapotangaziwa kushiriki kwenye makongamano yenye mafundisho, mikutano, na nafasi za ibada ili kujua mafundisho sahihi ya imani zao, kutumia imani hiyo katika maisha yao ya kila siku kutatua changamoto zinazowakabili katika familia na Taifa kwa ujumla .

Mhashamu  Christopher Ndizeye, Askofu wa Jimbo la Kahama alisema hayo leo katika Adhimisho la Misa Takatifu ya kutoa Sakramenti ya Kipaimara katika Parokia ya Mtakatifu Stephano Shahidi Nyasubi Kahama.

"Tupende kujua imani yetu, tupende kujua kanisa linatufundisha nini, na sisi kama  kanisa tunapenda kuongeza vipindi shuleni lengo kuu ni kusaidia wanafunzi wajue nini kanisa linataka wajue," alisema. 

Mbali na hilo, alishauri waumini watafute nafasi za  kujua ukweli kuhusu imani yao, mafundisho sahihi ya  imani yao na kuweka katika maisha Yao ya kila siku, kama Mtakatifu   Stephano alivyojua imani yake na hatimaye akakubali kufa kwa sababu alijua huu Ndiyo ukweli kuhusu imani yake.

Alisema kanisa limekuwa likiandaa mikutano, kongamano na ibada  mbalimbali zinazotoa mafundisho ya kiimani, lakini watu wanakuwa wazito kuhudhuria, waumini jitahidi kutafuta  nafasi ya  kujua mafundisho sahihi ya imani.

Lakini Pia  ukijua mafundisho ya imani haitoshi, najua waumini mnajua sala nyingi sana kuanzia sara ya asubuhi  hadi sara za jioni, lakini  lazima twende hatua  mbele, tunatumiaje imani yetu na sala tunazozijua katika maisha ya mwanadamu,  katika maisha yetu ya kila siku?  tunaitumiaje imani yetu kuleta amani katika familia zetu,  kutatua changamoto tulizonazo katika familia zetu,  kutoa haki na masuala mengine?  Alihoji Askofu Ndizeye. 

"Tunapozungumzia Sakramenti ya Ekaristi Takatifu, tunaalikwa kula  chakula cha kiroho kila siku,  lakini kabla ya kula tunatakiwa kujichunguza, kuwa wasafi , lazima uungame usije kupokea hukumu yake," alisema Aliomba watoto waliopata Sakramenti ya Kipaimara kujua amri za Mungu, wachukue walichofundishwa wakiweke kwenye maisha yao ya kila siku. 

Alisema katika ulimwengu tuliyonao sasa hivi, ukiona unasifiwa sana ujue unachukiwa, mimi natamani tuchukiwe, kama kuna  kinyume na misingi ya Kanisa Katoliki, tusimamie ukweli.  "Tuishi maisha halisi, siyo maisha ya kufikilika, hivi hofu tulizonazo watanzania, hivi kweli hakuna wakatoliki wanaosababisha hofu hizi?  tuombe Mwenyezi Mungu atusaidie katika changamoto hii ili watanzania waweze kuishi kwa  amani, wasiwe na hofu. 

Aliwambia waumini kuwa, kama hawathamini Ekaristi Takatifu  hakuna kitu,kwa sababu  yote tunayoishi na kuyatenda  yanatokana na Ekaristi Takatifu. Aliomba wakatoliki waliopo katika mazingira ya ngazi za serikalini, wawe wa shauri wazuri, wasikubali kila agizo linalotolewa, kama mamlaka hazikufundishi kutenda haki usifuate. 

Lakini Pia  kama Kuna changamoto zozote katika familia zetu, katika nchi yetu tukubali kushuka, tujadiliane, tuone tuna matatizo gani, tusimamie maadili ya dini yetu, lazima ukweli na haki visimame, tukubaliane kama hiki ni kibaya tukiache, kama ni kizuri tukifanyie kazi, watu wengi wana hofu.