Biteko awaasa wakristo kuliombea taifa

By Mwandishi Wetu , Nipashe
Published at 12:13 PM Apr 20 2025
Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko(katikati) akiwa na
mkewe Bernadetha katika ibada ya Pasaka katika Kanisa la African Inland Church (AICT), Makongoro jijini Mwanza
Picha: Mpichapicha Wetu
Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko(katikati) akiwa na mkewe Bernadetha katika ibada ya Pasaka katika Kanisa la African Inland Church (AICT), Makongoro jijini Mwanza

NAIBU Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dk. Doto Biteko, amewaasa wakristo kuliombea taifa amani, utulivu, umoja na mshikamano uendelee, ikiwa ni kuelekea uchaguzi mkuu Oktoba, mwaka huu.

Biteko amesema hayo leo, Aprili 20, 2025 jijini Mwanza, wakati aliposhiriki ibada ya Pasaka katika Kanisa la African Inland Church (AICT), Makongoro.

“Mwaka huu ni wa uchaguzi na una michakato mbalimbali ya kujiandikisha, kugombea, kupiga kura na kutangaza matokeo. 

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dk. Doto Biteko akizungumza wakati wa Ibada ya Pasaka katika Kanisa la AICT Makongoro jijini Mwanza
“Kwa niaba ya serikali napenda kuwaomba waumini wa AICT na wale ambao tunadhani tuna uwezo wa kugombea nafasi mbalimbali tujitokeze kwa wingi tugombee, wale tu wenye nia ya kweli tuhakikishe tunawasaidia watu katika hali zao,” amesema Dk. Biteko.

Sambamba na kugombea amewahimiza waumini kuliombea Taifa kuelekea wakati na baada ya uchaguzi “Tujitokeze ili tuweze kugombea, kwa ajili ya kuhudumia nchi yetu na wakati wa kampeni utakapofika naomba tuendelee kuliombea taifa,”

Waumini wa Kanisa la AICT Makongoro, jijini Mwanza wakiwa kwenye Ibada ya Pasaka iliyofanyika Aprili 20, 2025
Ameongeza kuwa Mwalimu Julius Nyerere na viongozi wengine waliweka misingi imara ya amani na kushikamana wakati wote na Tanzania, inafahamika duniani kote kama kisiwa cha amani hivyo waumini hao waliombee Taifa pamoja na Rais Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa anayoendelea kufanya katika taifa na kuendelea kufanya nchi kuwa na amani.

 “Tuliyofundishwa kwenye ibada ya leo, ni pamoja na kuwa ilikuwa kusudi la Mungu kwa Yesu afufuke na tunamshukuru Mungu, kwa ajili ya siku ya leo ya kutufanya kuwa hai na sisi waumini wa Kanisa hili kukutana hapa na kuabudu kwa pamoja,”

Pamoja na hayo Dk. Biteko amewaeleza waumini wa Kanisa hilo kuwa kufufuka kwa Yesu ni ishara ya ushindi na kuwa wote wameshinda pamoja na Yesu, kama alivyoshinda mauti, watashinda pia katika kukamilisha ujenzi wa kanisa lao ambalo wanaendelea kulijenga.

Askofu Mkuu wa AICT, Musa Magwesela, amesema waumini hao watumie nafasi ya kufufuka kwa Yesu, kwa kuleta mabadiliko katika maisha yao.

Awali akihubiri katika ibada hiyo, Mchungaji wa AICT kutoka Turkana nchini Kenya, Stephen Kilel, amesema kuwa tukio la Yesu kufufuka, ni tukio kuu linalowapa ujasiri wa kujua imani yao ni thabiti.

“Wapo watu wengine ambao hawaamini kama Yesu amefufuka. Sisi tunaweza kupata matumaini makubwa kumbe maisha yetu hayaishi pale ambapo kifo cha mwili kimetupata, kuna ufufuo ambao unatupa nguvu ya kuzungumza juu ya habari njema,” amesema Mchungaji Kilel.