Chama cha Ukombozi wa Umma (CHAUMMA) kimetangaza kushiriki Uchaguzi Mkuu wa 2025, kikisisitiza umuhimu wa Serikali kufanya marekebisho kwenye Tume Huru ya Uchaguzi ili kuhakikisha uchaguzi unakuwa huru na wa haki.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Mbeya, Katibu wa Habari na Uenezi wa CHAUMMA, Ipyana Samson, amesema ushiriki huo ni fursa ya chama kujipima na kubaini maeneo yenye changamoto.
“Tutashiriki kikamilifu kwenye uchaguzi ujao. Tunataka kuona namna chama kinavyopokelewa na wananchi katika kipindi hiki muhimu,” amesema Samson.
Aidha, amesisitiza kuwa CHAUMMA ni chama huru na hakiendeshwi kwa misimamo ya vyama vingine, bali kwa mujibu wa katiba na kanuni zake.
Katika kuelekea uchaguzi, CHAUMMA kimetoa mapendekezo ya marekebisho kwenye Tume Huru ya Uchaguzi, yakiwemo uteuzi wa makamishna, wakurugenzi wa halmashauri na wasimamizi wa vituo vya kupigia kura, ili kurejesha imani ya wananchi katika mchakato wa uchaguzi.
Kuhusu mgombea urais, chama hicho kimesema jina bado halijatajwa rasmi, huku mkutano mkuu wa chama ukitarajiwa kufanyika mwezi Juni kwa ajili ya uteuzi wa mgombea huyo.
© 2025 IPPMEDIA.COM. ALL RIGHTS RESERVED