MRADI EACOP; Wananchi zaidi ya 26,000 wanufaika na maji

By Mwandishi Wetu , Nipashe
Published at 09:24 PM Jul 17 2025
Muonekano wa utunzaji wa mazingira kwenye chanzo cha Mto Sigi mkoani Tanga
Picha: Mpigapicha Wetu
Muonekano wa utunzaji wa mazingira kwenye chanzo cha Mto Sigi mkoani Tanga

IMEELEZWA kuwa mradi wa ujenzi wa bomba la Mafuta ghafi la Afrika Mashariki (EACOP), hauna athari za kimazingira kutokana na serikali kuweka sera nzuri na teknolojia rafiki kwa mazingira, ili kulinda bayoanuai wakati wa upitishaji wa bomba la mradi chini ya Mto Zigi

Mhandisi Thomas Mhando, ambaye ni msimamizi wa mradi  wa ujenzi wa bomba kuvuka Mto Sigi, kinachojumuisha ulazaji wa bomba na uchorongaji kwa ajili ya kuvusha bomba chini ya mto , ameelezea maendeleo ya mradi kwenye eneo hilo, sambamba na kuhakikisha mazingira yanalindwa kipindi chote cha kusimika bomba hilo 

Mafundi kutoka kampuni ya CPP kutoka China wakiwa wanaendelea na ujenzi wa bomba linalopita chini ya mto kwenye kipande namba 16 mradi wa EACOP
Amesema wakati wa utekelezaji wa shughuli za ujenzi wa bomba linalopita chini ya mto, suala la uhifadhi wa mazingira limepewa kipaumbele cha hali ya juu sambamba na kutoa elimu kwa wananchi juu ya utunzaji wa vyanzo vya maji hasa cha Mto Sigi, kwani ndio tegemeo kwa wananchi wa Tanga na mradi wa EACOP kwa ujumla, ambacho kinahudumia takribani watu 26,552 ambao wanapatiwa maji na mamlaka ya maji Tanga.

Ameongeza kuwa, wakati wa utekelezaji wa mradi kupeleka maji EACOP, walikubaliana kuwawezesha pia wananchi wa vijiji saba vilivyoko karibu na maeneo ya  utekelezaji wa mradi kwa kuhakikisha wanapatiwa maji chini ya mradi wa makubaliano, jumla ya Sh. bil 2.728 zilitolewa na EACOP kutekeleza mradi wa maji ili wananchi pia wapate maji.

Awali akizungumza kwenye eneo la utekelezaji wa mradi huo, Mratibu wa kitaifa wa Mradi kutoka TPDC, Asiadi Mrutu, amesema kwa sasa uvushaji wa bomba kwenye Mto Sigi unaendelea vizuri na umefikia asilimia 63 na unatarajiwa kukamilika Novemba 2025 na ameishukuru NEMC kwa kusimamia suala la mazingira kwenye mradi huo kwa kuhakikisha wanatembelea mara kwa mara, ili kuona kazi inavyoendelea.
Muonekano wa utunzaji wa mazingira kwenye chanzo cha Mto Sigi mkoani Tanga
Mhandisi kutoka Kitengo cha Miradi Tanga Uwasa, Mhandisi Aaron Chanimbaga, ameishukuru EACOP kwa kuhakikisha wananchi wanafikiwa na huduma ya maji saa 24 tofauti na ilivyokuwa awali na bomba hilo lina uwezo wa kutoa lita za ujazo milioni 1.7 kwa siku na linahudumia wananchi wa Chongoleani, Ndaoya, Putini, Elani, Mleni, Mabokweni,na Kibafuti.

Ameishukuru serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, kwa ujio wa mradi kutoka Hoima nchini Uganda hadi Chongoleani mkoa wa Tanga na kueleza kuwa umeleta mabadiliko ya kiuchumi kwa mkoa wa Tanga.