DC Nyamwese atoa onyo kwa madereva wazembe

By Mwandishi Wetu , Nipashe
Published at 07:53 PM Dec 24 2025
 DC Nyamwese atoa onyo kwa madereva wazembe
Picha: Mpigapicha Wetu
DC Nyamwese atoa onyo kwa madereva wazembe

Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Salum Nyamwese, ameongoza Kikosi cha Usalama Barabarani wilayani humo kufanya ukaguzi wa kushtukiza katika barabara kuu ya Dar es Salaam–Tanga, eneo la Segera, ambapo jumla ya madereva 60 walibainika kukiuka makosa mbalimbali ya usalama barabarani.

Akizungumza wakati wa ukaguzi huo,  Nyamwese amesisitiza umuhimu wa madereva kuzingatia sheria na kanuni za usalama barabarani, hususan katika kipindi hiki cha msimu wa sikukuu, ili kuepusha ajali na kulinda maisha ya abiria pamoja na watumiaji wengine wa barabara.

“Ninatoa wito kwa madereva wote; huu ni msimu wa sikukuu, tafadhali epukeni kabisa matumizi ya vilevi mnapokuwa barabarani. Tuko macho saa 24. Dereva yeyote atakayekamatwa akiendesha gari akiwa amelewa katika barabara yetu hatapata msamaha, leseni yake itafutwa,” amesema Nyamwese.

Ameeleza kuwa ukaguzi huo ni sehemu ya jitihada za Serikali ya Wilaya ya Handeni katika kuhakikisha usalama wa wananchi unaimarishwa na ajali za barabarani zinapungua, hasa katika kipindi cha sikukuu.